https://monetag.com/?ref_id=TTIb Maelfu wajitokeza kuwaga mwili wa Robert Mugabe | Muungwana BLOG

Maelfu wajitokeza kuwaga mwili wa Robert Mugabe

Maelfu ya watu wanatoa heshima zao za mwisho kwa rais wa zamani wa Zimbabwe Robert Mugabe, katika uwanja wa taifa wa michezo mjini Harare hii leo Jumamosi.

Kulingana na msemaji wa rais George Charamba, viongozi 11 wa Afrika wanatarajiwa kufika katika uwanja huo unaoweza kuwakimu hadi watu 60,000.

Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa, rais Uhuru Kenyatta wa Kenya na rais wa Mozambique Filipe Nyusi ni miongoni mwa viongozi waliothibitisha kufika katika maziko hayo.

Mugabe alifariki wiki iliyopita nchini Singapore akiwa na miaka 95. alipinduliwa madarakani mwaka 2017 baada ya kuiongoza nchi hiyo kwa takriban miongo minne.

Wakati wengi wanasifu mchango wake katika kuikomboa Zimbabwe dhidi ya utawala wa watu weupe, baadhi wanamdharau na kuamini yeye ndie aliyesababisha uchumi wa Zimabawe kudidimia.

 Rais Emmerson Munangagwa hapo jana Ijumaa alisema Robert Mugabe atazikwa mwezi Ujao katika makaburi ya kitaifa ya mashujaa, baada ya kukamilika kwa ujenzi wa kaburi lake.

Mwili wake utapelekwa nyumbani kwake katika kijiji cha Zvimba hapo kesho kwa tambiko za kitamaduni.