Wadau wa maendeleo watakiwa kuunga mkono jitihada za Serikali


Na Thabit Madai, Zanzibar

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Riziki Pembe Juma amewakata wadau mbali mbali wa maendeleo   nchini kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) katika kuinua sekta ya Elimu.


Amesema wadau hao kama vile taasisi za kibenki wanatakiwa kuwa mstari wa mbele katika kuinua sekta ya elimu ili Taifa liwe na wataalamu wengi wa kila fani.

Kauli hiyo ameitoa jana katika hafla ya kuwazadia Wanafunzi wa Kidato cha Sita waliofaulu daraja la kwanza katika masomo ya Sayansi na Biashara katika ukumbi wa Hoteli  ya Abla  uliopo Beit el Arasi Mkoa wa Mjini Maghribi Unguja,

Zawadi hizo zimetolewa na Benki ya watu wa Zanzibar (PBZ) kwa wanafunzi 188 waliofaulu kwa kiwango cha daraja la kwanza masomo ya Sayansi ya Biashara.

Waziri Pembe alisema kuwa wadau mbali mbali hawana budi kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuinua sekta ya elimu nchini ili taifa liwe na waalamu mbali mbali wa kutosha.

Alisema Benki ya watu wa Zanzibar PBZ  kuwazawadia wanafunzi waliofanya vizuri ni jambo la kuingwa na wadau wote wa maendeleo nchini ili kutoa hamasa kwa wananfunzi mbali mbali kuongeza bidii na kufaulu mitihani yao.

“Jambo la kuwazadia Wanafunzi 188 waliofaulu daraja la kwanza ni Jambo la kupigiwa mfano na kupongezwa, kwani hayo ni miongoni mwa kuwafanya watoto waweze kusoma kwa bidii na kuleta ufanisi mzuri katika sekta ya Elimu nchini,” alisema Waziri Pembe .

Pia alisema  kuna umuhimu wa kuzawadiwa na Walimu wao Kwani wao ndio chanzo cha ufaulu huo kutokana na juhudi zao paoja na kutumia mbinu Mbadala ili kuhakikisha  wanafunzi hao wanapata matokeo mazuri.

Aidha  Riziki aliwataka  Wanafunzi hao kutoridhika na bidii hizo na badala yake waongeze kasi ya kusoma kwa lengo la kusonga mbele zaidi.

Hata hivyo  Riziki aliwataka Wanafunzi kulinda Mila na Tamaduni zao pindi watakapoanza masomo yao ya Elimu ya juu ambapo kutawapelekea kuweza kuepukana na vishawishi vitakavyoweza kuwaharibia masomo yao.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Watu wa Zanzibar PBZ Bi Khadija Shamte Mzee amesema  Benki yao itaendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuhakikisha Zanzibar inapiga hatua katika maendeleo ya Nchi.

Aidha aliwataka vijana kutumia njia nzuri za utunzaji fedha kwani  kutawapelekea kuwa na muelekeo mzuri wa kujiendeleza pamoja na kuepukana na tamaa.

Aidha aliwashauri Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar kuingiza somo la Elimu ya Fedha katika mitaala yake kuanzia ngazi ya msingi ili kuwasaidia watoto kujua namna ya utunzaji wa fedha na kuweza kuinua uchumi wa nchi.

Nae Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi  Ayoub Mohamed Mahmoud ameipongeza Benki ya watu wa Zanzibar PBZ pamoja na wadau mbalimbali wa Elimu kwa kuunga mkono jitihada za Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein katika kuinua kiwango Cha Elimu nchini.

Aidha aliwapongeza Wanafunzi wa Mkoa  wake kwa kutoa ufaulu mkubwa kwa Zanzibar nzima pamoja na wanafunzi wote waliofaulu na kuwataka kuongeza bidii zaidi huku serikali ya Mkoa wake ikiendelea na mipango ya kutekeleza ahadi zake kwa wanafunzi hao waliofanya vizuri katika mitihani yao ya taifa.

Mapema mdau wa Elimu kutoka Green Light Foundation Salum Mussa Omar amesema juhudi wanazozionesha  Wanafunzi ni kubwa  hivyo ipo haja ya kupongezwa  kwa lengo la kuhakikisha wanakua na bidii katika Elimu ili Zanzibar kuibua wasomi na wataalam wa badae .

Benki ya watu wa Zanzibar PBZ, imetumia shilingi million 185 kwa ajili ya kuwazawadia Wanafunzi waliofanya vizuri waliopata daraja la kwanza kwa masomo ya Sayansi na Biashara pamoja na kuizawadia Skuli iliyofaulisha vizuri zaidi kwa kuipatiai komputa 15 , ikiwa ni miongoni mwa faida waliyoipata mwaka jana katika makusanyo yao.