Waziri Mwakyembe awapongeza Wazee wa Kimasai kwa kudumisha Mila


Waziri wa Habari, Utamaduni,Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe amepongeza wazee na viongozi wa kimila wa kabila la kimasai kwa kuendeleza na kuhifadhi mila na desturi.

Hayo ameyasema leo Ngaramtoni, Jijini Arusha wakati wa kufunga mafunzo ya kimila kwa vijana wa kimasai na kueleza kuwa mafunzo hayo ni muhimu katika kumjenga kijana kuwa mtu mwenye maadili na kuheshimika kwa jamii yake.

“Mafunzo haya mliyoyapata kutoka kwa viongozi wenu na Wazee wa kimila yanawajenga kuwa rai wema na wenye maadili katika kujenga taifa letu ” Dkt. Mwakyembe

Aidha aliongeza kwa kueleza kuwa Wizara inaunga mkono juhudi zinazofanywa na Wazee wa Kimasai kwa kuhakikisha mila na desturi ya mtanzania inatunzwa na kuendelezwa kwa ajili ya vizazi vijavyo.

Pia Dkt. Mwakyembe ameahidi kushirikiana kwa karibu na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi katika kuhakikisha maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli za mila yanahifadhiwa vizuri bila kuingiliwa na watu.

Vilevile aliwapongeza viongozi wa Jeshi la Tanzania kwa kuruhusu maeneo ya kijeshi ambayo ni ya kihistoria kuendelea kutumika ajili ya masuala ya kimila na kuzitaka taasi nyingine ambazo zina maeneo hayo kuiga mfano huo .