Tembo sita wafa maji wakijaribu kuokoana

Tembo sita wameanguka na kufa nchini Thailand wakijaribu kuokoana katika mteremko hatari wa maji.

Maafisa wanasema kisa hicho kilitokea baada ya tembo mchanga kuteleza na kuanguka ndani ya mteremko wa maji katika mbunga ya kitaifa ya Khao Yai kusini mwa Thailand.

Wawili kati ya tembo hao wameonekana chini ya mlima ulio karibu huku mamlaka nchini humo ikijaribu kuwatoa mahali hapo.

Sio mara ya kwanza tembo kufa katika mteremko huo wa maji unaofahamika na wenyeji kama Haew Narok (Maporomoko ya jehanamu).

Tembo wanane walianguka na kufa katika eneo hilo mwaka 1992.

Maafisa wa kulinda wanyama na mimea wa Kitengo cha mbuga ya kitaifa ya Thailand, walifika katika eneo la tukio mapema Jumamosi baada ya kufahamishwa kuwa kundi la tembo limefunga bara bara karibu na eneo lenye mteremko wa maji.

Saa tatu baadae mzoga wa tembo wa miaka mitatu ulionekana chini ya mteremko wa Haew Narok, na mizoga mingine mitano ikapatikana karibu na hapo.

Edwin Wiek, mwanzilishi wa hazina ya kulinda maslahi ya wanyama pori nchi Thailand, amesema tembo hao hawangeliponea ajali hiyo kwasababu wengi wao hushirikiana kwa ulinzi na kutafuta chakula.

Mkasa huo utawaathiri tembo wengine katika mbuga hiyo.

"Ni sawa na kuondokewa na nusu ya familia yako," Bw. Wiek toldaliiambia BBC.

"Hakuna unachoweza kufanya, ndio hali ya dunia," aliongeza.

Karibu tembo 7,000 wa bara Asia wanapatikana nchini Thailand.