Baada ya bondia Hassan Mwakinyo usiku wa jana kumchapa Arnel Tinampay wa ufilipino kwa pointi, ametangaza kutamani kuwaona Manny Pacquiao na Amir Khan wanatua bongo kuzichapa.
Akiongea na Azam TV, baada ya kumalizika kwa pambano hilo, Mwakinyo alisema anatamani Manny Pacquiao na Amir Khan waje Tanzania acheze nao maana haamini kama kuna utofauti wa ngumi.
"Huu ni mwanzo tu, tunamtaka Manny Pacquiao na Amir Khan waje Tanzania hapa tucheze
nao. Mimi siamini kama kunautofauti wa ngumi, ngumi nilizocheza mimi ndio
alizocheza Mfilipino ingawa mimi nipo Tanga na yeye yupo Ufilipino kwa Manny
Pacquiao," amesema Mwakinyo.
Pia Mwakinyo amefunguka sababu ya kutofanya vizuri kwenye pambano lake la jana dhidi ya Tinampay huku akitaja sababu kubwa iliyomuangusha ni gloves alizovaa sio zile ambazo amezoea kupigana nazo.
"Niliamini kwenye ufiti wangu hajakutana na mtu anayeweza
kupiga. Nimegundua kitu kinachombeba siyo bondia mkali bali ni mvumilivu sana.
Hata mimi sijaridhika ila kwa sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu, kama unaona
kabla ya pambano kulikuwa na maongezi ya muda mrefu sana kwa sababu walikuwa
wanasema gloves nilizovaa hazifai. Nimevaa gloves ambazo sijazizoea sijawahi
kucheza nazo pambano lolote ni mara ya kwanza," amesema.
Mwakinyo ameongeza, "Siyo kama sijacheza vizuri ila nimeridhika kutokana na
mchezo jinsi ulivyokuwa unaenda, kwa sababu ningekuwa kwenye form yangu ile
ninayoitaka mimi ningekuwa huru kucheza na gloves ambazo nimezoea kucheza nazo."