CHADEMA yatoa msimamo mkali Uchaguzi Serikali za Mitaa


Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kupitia kwa Naibu katibu mkuu wake upande wa Tanzania bara, John Mnyika kimepiga marufuku jina na nembo yake kutumiwa na serikali kwenye nyaraka za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika Novemba 24.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema - Bara, John Mnyika amesema chama hicho kimejitoa kwa sababu ya dhuluma zilizofanyika kwenye mchakato mzima.

“Sisi kama chama tutamwandikia barua Waziri Jafo ya kumpiga marufuku kulitumia jina la Chadema au nembo yake katika mchakato wa uchaguzi kwa sababu tumejitoa,” John Mnyika.

Pia, amewataka wagombea waliopitishwa kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa kuendelea kuwasilisha barua za kujitoa kwa sababu ndiyo msimamo wa Kamati Kuu ya chama hicho.

Hata hivyo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Selemani Jafo amesema Mamlaka ya Uchaguzi inawatambua wagombea wa vyama vya upinzani vilivyotangaza kujitoa kwenye Uchaguzi huo.