Na John Walter-Kondoa-Dodoma
Naibu Waziri wa fedha na Mipango ambae pia ni Mbunge wa jimbo la Kondoa vijijini Dr. Ashatu Kijaji, ameliomba shirika la maendeleo la umoja wa mataifa (UNDP) kuwawezesha wakazi wa kijiji cha Pahi kilichopo Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma kuwajengea visima vitatu vya maji katika shamba la halmashauri ya Kondoa ambalo lipo ndani ya kijiji hicho kwa ajili ya kuwasaidia kulima kilimo cha umwagiliaji ili waweze kukilisha kiwanda kipya cha alizeti kilichojengwa kijijini hapo.
Ombi hilo limekuja mara baada ya kijiji hicho kujengewa kiwanda cha kisasa cha kukamua mafuta ya Alizeti pamoja na kununua Alizeti na shirika la maendeleo la umoja wa mataifa (UNDP) chenye thamani ya zaidi ya Million 51 kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wa eneo hilo kutokutembea umbali mrefu wa kutafuta huduma ya kukamua mafuta na kuuza alizeti.
‘’Ndugu zangu nimeulizwa hapa na Bi. Christina Msisi ambae ni mwakilishi mkaazi wa shirika la maendeleo la umoja wa mataifa kuwa tunamalighafi ya kutosha? Nimemjibu kwa nguvu zote hatuna kwa sasa alizeti ya kutosha ya kuweza kuchakatwa kila siku, na nimuombe mbele yenu tunaloshamba lenye zaidi ya Ekari 2,000 kata ya jirani lile shamba ni la halmashauri tunaomba ili mradi huu uwe kweli mradi wa kuongeza mapato ya halmashauri tuwezeshe kwenye shamba lile tupate japo visima vitatu tufunge miundombinu ya umwagiliaji ili tulime mwaka mzima alizeti na kiwanda chetu kifanye kazi mwaka mzima’’alisema Dr. Kijaji.
Chuo cha mipango vijijini kwa kushirikiana na shirika la maendeleo la umoja wa mataifa kimeamua kujenga kiwanda hicho ambacho kitawasaidia wananchi wa Kondoa kukamua mafuta lakini pia kuuza alizeti yao sehemu ya karibu bila kutumia gharama ya kusafirisha hadi mjini au kubaki kutegemea walanguzi ambao wamekuwa wakinunua alizeti hiyo kwa bei ya hasara na hii ni kuendana na mabadiliko ya tabia ya nchi ambapo lengo ni kuwatoa wananchi kwenye umasikini.
Kiwanda hicho kinauwezo wa kukamua na kuchunja mafuta tani 4 na nusu za alizeti kwa siku na mafuta yanayotoka baada ya kuchunjwa ni safi na salama kwa matumizi ya binadamu kutokana na kiwanda hicho kuwa na uwezo wa kupepeta kuondoa vumbi, mchanga, mawe pamoja na uchafu wowowte ambao umekuwa umechanganyika na Alizeti ikilinganishwa na viwanda vingine ambavyo havina uwezo wa kufanya hivyo.
Akizungumza katika uzinduzi wa kiwanda hicho Kaimu Mkurugenzi wa chuo cha Mipango vijijini kilichopo Dodoma Dr.Vedastus Timoth alisema kuwa kukamilika kwa kiwanda hicho ni moja ya utekelezaji wa adhima ya serikali ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda.
