Faida zitokanazo na ulaji wa parachichi kiafya

Parachichi ni tunda lisilo na ladha ya sukari linalopendwa na watu wengi. Watumiaji wanalitumia kwa namna tofauti.

Wapo wanaokula baada ya kulimenya, wengine hulitengenezea juisi huku wengine wakilitumia kula kama mboga kwa kulichanganya kwenye vyakula hususan wali.

Tunda hilo lenye virutubisho vingi na muhimu kwa afya ya binadamu, linaelezwa na wataalam wa afya kuwa lina msaada mkubwa katika kulinda afya ya binadamu.

Parachichi linaelezwa kuwa ni mbadala wa vyakula vya nyama kwa jinsi lilivyo na malighafi zote zilizo muhimu ndani yake.

Tunda hilo linapotengenezwa kama kinywaji (juisi) husaidia kuondoa maumivu ya tumbo na kuponya vidonda vya tumbo pamoja na kurekebisha udhaifu mwingine tumboni.

Tunda hili linapotumiwa linasaidia kuongeza nguvu za mwili na ubongo sanjari na kujenga neva za fahamu. Pia linampa mtu uwezo wa kuona, huku majani yake yakielezwa kuongeza damu.

Si hivyo tu, majani hayo yamesheheni wingi wa vitamini A, B, C na E. Mandai anasema vyakula kama nyama vinasababisha 'asidi ya yuriki ' nyingi mwilini ambayo ni chanzo cha magonjwa mengi.

Tunda hilo likitumiwa kwa maelekezo ya kitaalamu linaweza kusafisha na kuitoa asidi hiyo na hivyo kumwacha mlaji katika uhakika wa kuondokana na tishio la magonjwa ambayo yangeweza kumpata.

Tunda hili hufanya vizuri kwa magonjwa hayo na kuyamaliza, lakini pia linasaidia wanawake  kuifanya hedhi iende vizuri kila mwezi,.

Pia majani ya parachichi yanapochemshwa na kunywewa kama chai yanasaidia kuondoa matatizo mwilini, ikiwa ni pamoja na uchovu, udhaifu na kujisikia ovyo, kuumwa kichwa, koo, tumbo, mapafu na uvimbe.

Hali kadhalika, unapotafuna majani yake husaidia kutibu vidonda vya mdomo (ufizi) na kuimarisha meno pamoja na kuondoa maumivu.

Pamoja na hayo, parachichi pia linaweza kutumika hata katika masuala ya urembo, linasaidia mwenye tatizo la nywele kukatika.

Mtaalam huyo anasema hizo ni baadhi tu ya faida nyingi za parachichi tunda linastawishwa kwa wingi zaidi katika mikoa kadhaa hapa nchini ukiwemo Kilimanjaro na Tanga.

Anatoa mwito kwa jamii kupenda kutumia matunda kutokana na umuhimu wake katika kulinda afya zao.