Breaking: Iran yakiri kudungua ndege ya Ukraine 'kimakosa'

Jeshi la Iran hatimaye limekiri kudungua "kimakosa" ndege ya abiria Ukraine siku ya Jumatano, runinga ya taifa ya Iran imeripoti.

Taarifa ya jeshi inaeleza kuwa mkasa huo umetokana na "makosa ya kibinadamu" baada ndege hiyo kupita karibu na eneo nyeti linalomilikiwa na Kikosi cha Mapinduzi (Revolutionary Guards).

Maafisa waliofanya kosa hilo wataadhibiwa, taarifa hiyo imeeleza.

Iran awali ilikanusha vikali taarifa kuwa moja ya makombora yake yaliitungua ndege hiyo karibu na mji mkuu Tehran.

Watu wote 176 ndani ya ndege hiyo wamepoteza maisha.


Iran awali ilikanusha vikali taarifa kuwa moja ya makombora yake yaliitungua ndege hiyo.
Hata hivyo nchi hiyo ilikabwa koo baada ya Marekani na Canada kudai kuwa taarifa za kijasusi walizonazo zinaonesha kuwa Iran iliidondosha ndege hiyo kwa bahati mbaya na moja ya makombora yake.

Kuanguka kwa ndege hiyo kulitokea saa chache baada ya Iran kushambulia kambi za kijeshi za Marekani nchini Iraq kwa makombora ya masafa marefu.

Vyombo vya habari vya Marekani vinadai kuwa Iran ilidhani kuwa ndege hiyo ilikuwa ya kivita ya Marekani, wakati taifa hilo lilipokuwa ikijiandaa kujibu mashambulio dhidi ya Marekani baada ya wao kushambulia vituo vyake vya kijeshi nchini Iraq kwa makombora.

Iran ilirusha makombora kwenye kambi za Marekani Jumatano kama sehemu ya kisasi chake baada ya rais Donald Trump kuagiza shambulio la anga lililomuua Jenerali wa Iran Qasem Soleimani Januari 3.

Kanda ya video iliyopatikana na gazeti maarufu la Marekani la New York Times ilionenesha jinsi makombora yalivyokuwa yakipita katika anga la Tehran na baadae kulipuka ilipokutana na ndege.

Karibu sekunde 10 baadae mlipuko mkubwa ulisikika ardhini. Ndege iliyoshika moto, inaendelea kupaa.

Rais wa Marekani Donald Trump siku ya Alhamisi alisema: "nina mashaka" juu ya (kuanguka) kwa ndege. "Inawezekana kuna mtu amefanya kosa kubwa."