Kampuni ya Ursino yachangia ujenzi wa miundombinu sekta ya Elimu



Na James Timber, Mwanza.

Kampuni ya Ursino jijini Mwanza imeunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya tano chini Rais Mhe Dkt John Magufuli ya kuboresha elimu kwa kuchangia gharama za ujenzi wa ofisi na miundombinu mengine katika shule ya Sekondari ya Kilimani manispaa ya Ilemela.

Akizungumza katika hafla ya kuwapongeza Walimu wa shule hiyo iliyofanyika katika viwanja vya Wagg Hill Luchelele, Mkurugenzi wa Kampuni ya Ursino Ltd Bwana Mnandi M. Mnandi amesema kuwa Kampuni yake inatambua jitihada za Serikali katika kuboresha sekta ya elimu na inaridhishwa na kasi ya Mhe Rais Dkt John Magufuli katika kuiimarisha sekta hiyo hasa kwa utaratibu wake wa kutoa elimu bure na kuimarisha miundombinu ya kujifunzia katika shule za Serikali ambazo ndizo zinazojumuisha watu wengi hasa wanyonge na wenye kipato cha chini,  Hivyo kuguswa na kuamua  kuisaidia shule ya Sekondari Kilimani kwa kuijenga ofisi ya Walimu, kuchangia gharama za maji na umeme shuleni hapo, sambamba na kugharamia safari za mafunzo kwa Walimu na wanafunzi katika maeneo mbalimbali ya kujifunzia nchini.


"Sisi kama Kampuni tunatambua juhudi za Serikali katika kuboresha sekta ya elimu hasa hii ya Mhe Rais Magufuli maana anafanya kama tulivyokuwa tunasoma sisi kipindi kile cha zamani kila kitu bure shuleni unaenda wewe
 tu, tuna kila sababu ya kuungua mkono jitihada hizi, " alisema

Aidha Bwana Mnandi ameiasa shule ya Kilimani kutobweteka na kuongeza juhudi ili kutokomeza sifuri shuleni hapo na kuwa na matokeo mazuri katika mtihani wa taifa wa kidato cha nne mwaka huu 2020 sanjari na kuwaahidi kuendelea kushirikiana nao kuhakikisha kero zote na changamoto zinatatuliwa.

Kwa upande wake afisa elimu wa manispaa ya Ilemela Bwana Emanuel  Malima ameipongeza Kampuni ya Ursino kwa uamuzi wake huo wa kuisaidia Serikali katika kupunguza changamoto zinazikabili shule hiyo na kuwaahidi ushirikiano, Ambapo mlezi wa shule hiyo Mwl Mugumba akiwataka Walimu hao kuongeza juhudi zaidi ili kupata matokeo bora yatakayoifanya shule hiyo kuwa ya kwanza kitaifa na kuwasisitiza kuwa inawezekana kama wataongeza bidii katika kuwajibika.

Kwa upande wake Mwalimu wa Taaluma wa shule hiyo Bwana Atanas Simon Manyika akiwasilisha taarifa ya kitaaluma amesema kuwa shule ya Kilimani imeshika nafasi ya pili katika matokeo ya mtihani wa taifa wa kidato cha nne mwaka huu kwa shule za Serikali ngazi ya mkoa,  Na kuwa shule ya 597 kati ya shule 3908 kitaifa pamoja na kutaja mikakati mbalimbali waliyojiwekea katika mwaka ujao ili kuvifanya shule hiyo kupata matokeo bora zaidi kwa mwaka wa masomo unaofuata.

Akihitimisha  Mwalimu mkuu wa shule hiyo Bwana Majaliwa Gerana ameishukuru Kampuni ya Ursino kwa kuisaidia shule yake huku akiomba wadau wengine wa maendeleo kujitokeza kuungana nao katika kuboresha sekta ya elimu.