Samatta akaribia kutua Aston Villa

Aston Villa inatumai kukamilisha makubaliano ya dau la £10m kumsajili mshambuliaji wa Genk Mbwana Samatta huku mkufunzi Dean Smith akilenga kuimarisha safu yake ya mashambulizi.

Dean anahitaji kuimarisha safu hiyo baada ya kumpoteza mshambuliaji wa Brazil Wesley kwa kipindi chote cha msimu kilichosalia na jeraha la goti alilopata katika mechi dhidi ya Burnley wakati wa siku ya mkesha wa mwaka mpya.

Samatta, ambaye alifunga dhidi ya Liverpool katika mechi ya klabu bingwa Ulaya msimu huu ameonekana kulengwa na Villa.

Hatahivyo maelezo ya ndani kuhusu uhamisho huo bado hayajaafikiwa.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 kutoka Tanzania anahitaji kibali cha kufanya kazi hivyobasi hatapatikana katika mechi ya ugenini ya Villa dhidi ya Brighton siku ya Jumamosi.

Villa iko tayari kumuuza mshambuliaji wa Ivory Coast Jonathan Kodija na tayari timu ya ligi ya mabingwa nchini England Nottingham Forest na ile ya Ligui 1 ya Ufaransa Amiens zikimnyatia .

Klabu hiyo ya Dean Smith ipo katika nafasi ya 18 katika ligi ya Premia baada ya kucheza mechi 22.

Villa pia imehusishwa na usajili wa mshambuliaji wa Leicester Islam Slimani mwenye umri wa miaka 31.

Mchezaji huyo wa Algeria kwa sasa yuko kwa mkopo akiichezea Monaco , na Smith alisema kwamba klabu hyo italazimika kujaribu kupata usajili.

''Mwezi wa Januari ni mgumu sana bila kuwepo na washambuliaji wazuri kwa kuwa klabu zinaweza kupandisha bei , limekuwa dirisha gumu la uhamisho na tutalazimika kufanya kitendo cha kijasiri'., alisema Smith.

''Mimi nimetulia na nina matumaini tutapata wachezaji lakini tuna mechi kubwa , na iwapo hatutapata mshambuliaji mmoja kufikia Jumamosi itakuwa mara ya tatu mfululizo bila mshambuliaji anayetambulika''..

''Lazima tuhakikishe kwamba tunafanya vyema na tunatumai tutapata mshambuliaji mmoja. Kuna haraka ya kupata mchezaji huyo''.

''Huku Wesley akipata jeraha na Keinan Davis akiwa nje lazima tujiimarishe vilivyo hivyobasi tunatafuta wachezaji kadhaa''.