Makamu wa Rais Samia Suluhu azindua mtandao wa viongozi Wanawake Afrika tawi la Tanzania

Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan amesema kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi za Jumuiya ya Maendeleo nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) ambazo zimepiga hatua katika kuwapatia Wanawake nafasi za uongozi na kufikia asilimia 36.7.

Hayo ameyasema leo jijini Dodoma  wakati wa uzinduzi wa Mtandao wa viongozi Wanawake Afrika tawi la Tanzania amesema nchi imekuwa ya 14 katika kuzindua tawi hilo na kesho nchi ya Uganda inatarajia kuzindua hivyo itakuwa nchi ya 15.

Mhe.Samia amesema kuwa kumekuwa na mabadiliko makubwa ya uwiano wa kijinsia ambapo kwa upande wa Bunge Kati ya wabunge 393, wanawake ni 126 ambao ni sawa na asilimia 36.7, na Baraza la Wawakikilishi la Zanzibar Wanawake ni asilimia 38.


“Ni kweli kuwa katika nchi nyingi duniani bado usawa wa kijinsia haujaweza kufikiwa katika nyanja mbalimbali ikiwemo ya uongozi,”amesisitiza Mhe.Samia

Hivyo hali kama hii inagusa pia Tanzania japokuwa kwa kiasi kikubwa imekuwa ikifanya vizuri kulinganisha na nyingine za bara la Afrika akitolea mfano mihimili mitatu ya Dola ambayo imekuwa na mabadiliko makubwa.

“Kiiwango hicho ni juu ya uwiano uliowekwa na nchi za SADC, Cha angalau asilimia 30, pamoja na hayo tulishakuwa na hayo, maspika wa mabunge wanawake hapa nchini na pia katika Bunge la Afrika, pia wanamanaibu spika Wanawake katika Bunge la Baraza la Wawakikilishi,”amesisitiza

Mhe.Samia amesema kuwa upande wa Mahakama, kuna majaji wanawake kwa Mahakama Kuu ni asilimia 30 na Mahakama ya Rufaa ni asilimia 38.


Samia amesema kuwa, katika Baraza la Mawaziri la wanawake ni asilimia 18 wakati Naibu Mawaziri ni asilimia 33,”kubwa zaidi na la kihistoria kwa Nchi yetu ni kuwa katika Serikali ya Awamu ya Tano, kwa mara ya kwanza nafasi ya Makamu wa Rais umeshikiliwa na mwanamke,”amesema.

Awali Mwenyekiti Mwenza wa Mtandao wa Viongozi Wanawake wa Afrika (AWLN) Tawi la Tanzania, Mary Rusimbi,amesema kuwa , umoja huo umeanza 2017 huku Tanzania ikiwa nchi ya 14 kuzindua na ulianzishwa kwa ushirikiano baina ya umoja wa mataifa na umoja Afrika.


Bi.Rusimbi amesema kuwa lengo kuu lilikuwa ni kuunganisha nguvu za pamoja Kati ya wanawake viongozi na wanawake.

Kwa upande wake Balozi wa Norway, Elizabeth Jacoben, amesema kuwa, kuwawezesha Wanawake kiuchumi na kisiasa ndio uchumi na malengo ya kimataifa na Norway wamekuwa wakitoa msaada mkubwa kuisaidia Tanzania katika masuala ya wanawake.

Naye balozi wa Sweden, Anders Sjoberg, amesema kuwa Duniani bado kuna changamoto mbalimbali za kufanya vitendo zaidi kuliko hotuba za maneno, na kwamba katika miaka 400 nchi hiyo wameweza kupata balozi 1 ambaye ni mwanamke.