Mawasiliano ni sehemu ya maisha ya Watanzania - Nditiye

Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye amesema kuwa huduma za mawasiliano ni sehemu ya maisha ya watanzania kwa kuwa wananchi wanahitaji mawasiliano na wametambua umuhimu wa huduma za mawasiliano nchini


Nditiye ameyasema hayo wakati akizindua mnara wa mawasiliano uliojengwa kwenye kijiji cha Mbunju Mvuleni kilichopo kwenye kata ya Mkongo iliyopo wilayani Rufiji mkoani Pwani uliojengwa na kampuni ya mawasiliano ya Halotel Tanzania kwa kutumia ruzuku ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayotolewa na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) ili kufikisha huduma za mawasiliano kwenye maeneo yasiyo na mvuto wa kibiashara na yaliyopo vijijini ambapo kampuni za simu haziko tayari kufikisha huduma za mawasiliano

“Sasa mawasiliano ni sehemu ya maisha ya watanzania, wanahitaji mawasiliano, UCSAF inatoa ruzuku kwa kampuni za simu na zinajenga minara ya mawasiliano, UCSAF imesaidia wananchi kuwasiliana,” amesisitiza Nditiye

Ameongeza kuwa ipo minara zaidi ya 68 ambayo tunahitaji izinduliwe ili wananchi wafahamu Serikali inatekeleza majukumu yake na ujenzi wa minara ni miradi mikubwa kwa kuwa ujenzi wa mnara mmoja gharama yake ni kati ya shilingi milioni 300 hadi milioni 400

“Hatutegemei umwone mtu anaharibu mnara huu mkakaa kimya kwa kuwa mnara huu ujenzi wake umegharimu shilingi milioni 320, hatutegemei mtu aende mbali kuuza bidhaa, utauza kwa simu na utapokea pesa kwa simu,” amesema Nditiye. 

Naye Mbunge wa Rufiji, Mohammed Mchengerwa ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kujenga minara ya mawasiliano ili kuwawezesha wananchi kuwasiliana kwa kuwa hapo awali wananchi wa kata ya Mkongo walikuwa wanapata changamoto ya huduma za mawasiliano na sasa mawasiliano yanapatikana, na huku ndiyo kwenye barabara inayokwenda kwenye eneo linakojengwa bwawa la Nyerere la Kufua Umeme

Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Juma Njwayo amemweleza Nditiye kuwa asilimia 80 ya eneo la Wilaya hiyo mawasiliano yanapatikana. “Leo wananchi hapa kijijini wananunua umeme kiganjani kwao kwa kutumia simu ya mkononi bila kwenda Ikwiriri,” amesema Njwayo.

Mwenyekiti wa Bodi ya UCSAF, Dkt. Joseph Kilongola wakati akiwasalimu wananchi wa Kata ya Mkongo alisema kuwa, “sisi kama bodi tunatekeleza maelekezo ya Serikali ya kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma za mawasiliano

Katika kipindi cha miezi miwili, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano inatarajia kuzindua minara ya mawasiiiano 68 iliyojengwa na ruzuku ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia UCSAF kwa kushirikiana na kampuni za siu za mkononi ili kuendelea kuhakikisha kuwa wananchi waishio maeneo yasiyo na mvuto wa kibiashara na vijijini wanapata huduma za mawasiliano