Wahamiaji Haramu 9 Wakamatwa Dodoma

Jeshi la Polisi Mkoani Dodoma linawashikilia watu wawili akiwamo Mwalimu wa Shule ya Sekondari Kifaru Kelvini Mpoli (39)Mkazi wa Himo, Kilimanjaro, na Cathbert Kirita (58) Mkulima na Mkazi wa Kilema Moshi kwa kosa la kusafirisha wahamiaji haramu 3 kutoka Kilimanjaro kwenda Songwe kupitia njia ya Dodoma.


Akizungumza na waandishi wa habari leo ofisini kwake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, SACP Gilles Muroto, amesema mnamo tarehe 14/02/2020, huko katika kijiji Cha Mtera Wilayani Mpwapwa, Mkoani Dodoma, walikamatwa wahamiaji haramu watatu ambao ni raia wa Kenya wenye asili ya Somalia.


"Wahamiaji haramu hawa watatu walikamatwa katika kijiji Cha Mtera Wakiwa wanasafirishwa na watanzania, wahamiaji hawa Wakiwa ni raia wa Kenya wenye asili ya Somalia waliingia nchini bila vibali, Kati yao Wanawake wawili na Mwanamme mmoja walikamatwa wakisafirishwa kwenye gari namba T. 248 AWA, Nissan Patrol rangi nyekundu".


Aliwataja wahamiaji haramu hao kuwa ni" Abdirahmani Mohamed (25), Luul Mohamed (30) na Hawa Gedow (18) wote Wakiwa ni Wasomali wenye uraia wa Nchini Kenya" amesema Kamanda Muroto.


Pia amesema mnamo tarehe 03/2/2020, katika kijiji Cha Chinene, Kata ya Haneti, Tarafa ya Itiso Wilayani Chamwino Mkoani Dodoma, katika njia ya Dodoma- Arusha, walikamatwa wahamiaji haramu sita (6) raia wa Somalia waliokuwa kwenye gari la abiria lenye namba T.858 DAP Mali ya Kampuni ya Capricorn, kutoka Arusha kwenda Mbeya.


Amesema wote walikuwa na hati za kusafiria kutoka Kenya lakini walitiliwa mashaka na kubainika waliingia nchini bila uhalali.