Kinondoni yaanza kupuliza dawa maeneo ya makusanyiko kupambana na corona


Halmashauri ya Manispa ya Kinondoni kwa kushirikiana na wataalamu wa Afya wa Halmashauri hiyo na mkoa wa Dar es Salaam wameendesha zoezi la upuliziaji dawa katika vituo vya mabasi yaendayo haraka pamoja na vituo vya daladala ikiwa ni katika mkakati wa kudhibiti  maambukizi ya Vizuri vya Corona.

 Zoezi hilo  limefanyika katika maeneo mbalimbali ikiwemo makazi ya wananchi , maeneo ya kutolea huduma mbalimbali ikiwemo masoko sambamba na kwenye mikusanyiko ya watu hususani  Kanisani na Msikitini.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mstahiki Meya wa Halmashauri hiyo, Mhe. Benjamini Sitta amesema kuwa zoezi hilo linafanyika kwa lengo la kuuwa wadudu wanaosababisha maambukizi ya Vizuri vya Corona (COVID 19) na kwamba maeneo yote katika Halmashauri hiyo yatapuliziwa dawa.

Meya Sitta amefafanua kuwa ugonjwa huo ambao umekuwa tishio kubwa duniani Halmashauri hiyo imejipanga kikamilifu katika kuukabili ugonjwa huo usisambae ikiwa ni pamoja na kusambaza wataalamu wa kupulizia dawa hiyo kwenye kata zote za Halmashauri hiyo.

“Kwa ujumla tunashiriki ipasavyo katika kupambana na maambukizi ya virusi hivi, kwa pamoja tunaunganisha nguvu kutoka kwenye ngazi ya mkoa,  Kinondoni ni Halmashauri moja wapo ambayo imeanza zoezi hili  kwenye maeneo yote na leo tumeanzia Kata ya Msasani ambapo ndio kuna wataalii wengi” amesema Mhe. Meya Sitta.

Mhe. Meya Sitta ameongeza kuwa “ ni jambo la muhimu kuchukua hatua kabla ya kupata madhara , nakinga ni muhimu kuliko tiba , Kinondoni hatujasubiri janga hili litufikie, tulianza kuchukua hatua mapema, tulijiandaa vizuri ndio mana hata sasa tunaendelea kuchukua hatua kwakupiga dawa kwenye maeneo ya wananchi wetu.

Aidha Mhe. Meya Sitta amesisitiza kuwa Kinondoni imejipanga na hivyo kuishukuru Serikali ya awamu ya tano kwakudhibiti na kupambana dhidi ya kutokomeza ugonjwa huo sambamba na kuwaelimisha wananchi jambo ambalo limepokelewa kwa asilimia 100.

Kwa upande wake Mratibu wa Malaria mkoa wa Dar es Salaam, Dokta Ford Chisongela amesema kuwa  mkoa unashirikiana na Halmashauri katika kuhakikisha kuwa unatokomeza ugonjwa huo unaosababishwa na Vizuri vya COVID 19 ( Virusi vya Corona) kwa kupulizia dawa hizo katika maeneo yote ya mkoa huo.

Amefafanua kuwa katika kuongeza nguvu ya kupulizia dawa hiyo, mkoa umeamua kutumia magari ya zimamoto pamoja na yale ya Polisi kikosi Cha kutuliza ghasia (FFU) kwa lengo la kuongeza nguvu katika zoezi hilo kwa kuwa magari hayo yanauwezo mkubwa wa kufanya kazi  kwa haraka na hivyo kuwatoa hofu wananchi wasishtuke pindi watakapo yaona mitaani.