Akifunga kīkao cha Bunge jioni ya leo, Ndugai ametangaza kuwa mazishi ya Rwakatare yatafanyika Alhamisi ya Aprili 23, 2020 na yatahudhuriwa na watu wasiozidi kumi, pia familia imeomba azikwe kwenye eneo la Kanisa Mlima wa Moto.
“Familia ya marehemu Mama Rwakatare imeomba mambo mawili serikalini, ikiwezekana mama yao azikwe kwenye eneo la Kanisa la Mlima wa Moto, pia wameomba iwe kesho kutwa Aprili 23. Serikali imekubali na itasimamia mazishi hayo ambayo washiriki hawatazidi kumi,” amesema Ndugai.
Ameongeza kuwa wabunge hawatamuaga mbunge huyo mwenzao, kwa utaratibu uliokuwa ukitumika siku zote kutokana na mazingira halisi ya sasa.
Akizungumza bungeni leo, Aprili 21, 2020, amesema kuwa kwa kawaida mbunge anapofariki Bunge huahirisha kikao kimoja na kisha humleta katika maeneo ya bunge na kumuaga kabla ya kupelekwa kwenye makazi yake ya milele. Lakini kutokana na tishio la kusambaa kwa virusi vya corona, utaratibu huo hautatumika.
Hata hivyo, alisema kuwa Bunge liliahirisha kikao kimoja kwa ajili ya kuomboleza kifo cha mbunge huyo.
“Mazingira ya sasa hayaruhusu kufanya zoezi hilo. Kwa hiyo, hatutaweza kumleta mwenzetu hapa kwa sababu ya hali halisi tuliyonayo,” amesema .
“Maelezo mengine tutayapata kesho baada ya kuwa tumemaliza mazungumzo kati ya ofisi ya Bunge na familia ya marehemu wakati Serikali nayo ikijiandaa kusaidia pale ambapo tunaweza kuomba msaada wowote ambao utahitajika,” aliongeza.
Katika hatua nyingine, Spika aliwasihi wabunge kuhakikisha kuwa wanapojisikia hali isiyo ya kawaida kiafya wasijilazimishe kufika bungeni kwa hofu ya kutokiuka utaratibu, kwani mazingira ya sasa yanafahamika.
Dkt. Rwakatare ambaye alikuwa Askofu Kiongozi wa Kanisa la Mlima wa Moto alifariki alfajiri, Aprili 20, 2020 akiwa na umri wa miaka 70. Mwanaye alieleza kuwa alifariki kutokana na tatizo la moyo.