Maddam Rita Amlipa Meshack Mil 5/-

MUANDAAJI wa shindano ya kusaka vipaji (BSS), Rita Paulsen, ameanza kumlipa mshindi wa mwaka 2019, Meshack Fukuta, kama alivyoamriwa na serikali.

Juzi Rita na Meshack ambaye alidai kudhulumiwa fedha alizoahidiwa kama mshindi, walikwenda Baraza la Sanaa Tanzania (Basata) na kulipwa Sh milioni 5 mbele ya Katibu Mtendaji wa Baraza hilo, Godfrey Mngereza.

Akizungumza jana, Meshack alishukuru BSS kwa kuanza kumlipa fedha zake na kuishukuru serikali na Basata kwa jinsi walivyomsaidia na elimu waliyompatia, pia BSS kwani imemtoa chini hadi sasa ni msanii anayejulikana na anatarajia kufanya makubwa.

“Watu wanauliza pesa sana, nashukuru wameanza kunilipa na wataendelea, lakini watu wanatakiwa wasiangalie sana kwenye pesa maana kupitia shindano hili nimepata faida nyingi, BSS ilipata changamoto, lakini leo wameanza kunilipa naamini wataendelea kunilipa,” alisema Meshack.

Pia aliwapa moyo washiriki wengine wasiogope changamoto, kwani ni sehemu ya mafanikio na kuzitumia kama fursa. Naye Rita alisema wataendelea kumlipa msanii huyo kwa jinsi atakavyokuwa anapata fedha na kueleza watakuwa wanaingiza kwenye akaunti yake.

“Atalipwa pesa yake yote, nitaingiza kwenye akaunti nikipata hata leo nampa yote, mimi ni mzungu wa roho,” alisema Rita.

Pia alisema walikuwa waanze matangazo ya msimu wa 2020 mwezi huu, lakini kutokana na janga la corona wanasikilizia na kama mfadhili atasema waendelee kwa kufuata teknolojia bila kukusanya watu wataanza.

Aprili 8, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Juliana Shonza, alitoa mwezi mmoja kwa waandaji wa BSS kuhakikisha wamemlipa mshindi wa kwanza wa mashindano hayo ya mwaka 2019 kama walivyoahidi kutoa zawadi hiyo ya kiasi cha Sh milioni 50.

Mashindano hayo BSS yalifanyika Desemba 24, 2019, Dar es Salaam na kwa mujibu wa mkataba, Meshack atalipwa Sh milioni 20 na Sh milioni 30 zitatumika katika kusimamia kazi zake kwa mwaka mmoja.