Madiwani Sikonge waomba serikali kuitaka JUHIWAI kutumia EFD kwenye makusanyo


BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge wameuomba Uongozi wa Mkoa wa Tabora kuiagiza Jumuiya ya Uhifadhi wa Wanyamapori Ipole(JUHIWAI) kutumia Mashine za Risiti za Kielektroniki (EFD)wakati wa makusanyo ya fedha mbalimbali wanayofanya.



Kauli hiyo imeolewa jana na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge Peter Nzalalila wakati kikao cha Baraza la Madiwani cha robo ya tatu.



Alisema ni vema Mkoa ukasaidia kuondoa tatizo la JUHIWAI kutotumia mashine za EFD wala POS katika makusanyo yanayofanyika katika Jumuiya hiyo ili kuiepushia Serikali kupoteza mapato yake.



Nzalalila alisema ni vema Jumuiya hiyo ikalazimishwa kutumia mashine ya kukusanyia  mapato ya Serikali badala ya kutumia stakabadhi.







Alisema kitendo cha Jumuiya hiyo kuendelea kutotumia pos wala EFD, Serikali imekuwa ikipoteza mapato mengi kwa kuwa hajulikani kiasi wanachokusanya.



Kwa upande wa Katibu Tawala Mkoa wa Tabora Msalika Makungu alisema Serikali ya Awamu ya Tano ilishaagiza mapato yote ni lazima yakusanywe kwa mashine ya kielektoniki.



Alisema atawasiliana na Wizara ya Maliasi na Utalii ili kuhakikisha Jumuyia hiyo inaweka Mfumo wa Mashine za Risiti za Kielektroniki (EFD) ili kulinda mapato ya Serikali yasipotee.



Makungu aliongeza kuwa katika maeneo mbalimbali ambayo yameweka mfumo wa Mashine za Risiti za Kielektroniki (EFD) mapato ya Serikali yameongezeka hadi mara tatu waliyokuwa wakikusanya kwa kutumia stakabadhi za karatasi.



Alisisitiza kulifuatilia tatizo hilo la kulipatia ufumbuzi haraka na kuwapa taarifa katika kikao kijacho cha Baraza la Madiwani.