Vyuo Tanzania vyatakiwa kufidia muda wa masomo

WIZARA ya Elimu, Sayansi na Teknolojia nchini Tanzania imevitaka vyuo vikuu nchini humo kujiandaa kikamilifu ili kukamilisha mitaala pindi vyuo vitakapofungiliwa tarehe 1 Juni, 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).

Hayo yamesemwa leo Jumamosi tarehe 23 Mei, 2020 na Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dk. Leonard Akwilapo wakati akifungua kikao kilichowakutanisha Wakuu wa Vyuo Vikuu vyote nchini humo chenye lengo la kuweka mkakati wa pamoja wa namna ya kufikia malengo ya ufundishaji na ukamilishaji wa Mitaala pindi Vyuo vitakapofunguliwa.

Vyuo hivyo vinafunguliwa baada ya kufungwa tarehe 18 Machi, 2020 kutokana na maambukizi ya corona.

Akifungua kikao hicho kilichofanyikia jijini Dodoma, Dk. Akwilapo amesema pamoja na mambo mengine  wamekubaliana namna bora ya kuhakikisha vyuo vinafidia muda wa masomo uliopotea na kukamilisha mihula bila kuathiri taaluma.

Mengine yaliyojadiliwa katika  kikao hicho ni kuhakikisha vyuo vinawasilisha nyaraka zote muhimu ili wanafunzi wapate mikopo yao mapema vyuo vitakapofunguliwa.

“Hakikisheni katika vyuo vyenu  mnachagua maafisa mikopo ambao watatoa ushirikiano mzuri kwa wanafunzi ili kusiwe na malalamiko wakati wa kushughulikia mikopo yao,” amesema Dk. Akwilapo.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Makamu Wakuu wa Vyuo, Marasi na Maprovosti Tanzania (CVCPT), Profesa Raphael Chibunda amesema wanaishukuru wizara kwa kuitisha kikao hicho ili kuweka mipango kwa pamoja utakaowasaidia kufungua vyuo bila changamoto.

Profesa Chibunda ambaye pia ni Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), amesema vyuo tayari vimejipanga  kuhakisha jumuiya za vyuo zinakuwa salama dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona kwa kuzingatia  maelekezo ya wataalamu wa afya huku wakiendelea na masomo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu, Abdul-Razaq Badru amesema Bodi imejipanga kutoa mikopo kwa wanafunzi kwa wakati kwa kushirikiana na vyuo huku akivishauri vyuo hivyo kushirikiana na uongozi wa wanafunzi wakati wa zoezi la utoaji mikopo ili kurahisisha utekelezaji wa kazi hiyo.