Bunge nchini China limeipitisha sheria kali ya usalama wa taifa kwa ajili ya jimbo lake la Hong Kong hivi leo, katika hatua ya kihistoria ambayo wakosoaji na serikali nyingi za Magharibi zinahofia kuwa zitaupoka uhuru na mamlaka za kituo hicho kikuu cha fedha ulimwenguni.
Kwa kauli moja, bunge la China ambalo wengi wanalichukulia kuwa ni mdomo tu wa serikali na chama tawala, liliipitisha sheria hiyo, chini ya wiki sita baada ya kusomwa kwa mara ya kwanza.
Mwanaharakati mashuhuri wa demokrasia, Joshua Wong, ameandika kwenye mtandao wa Twitter kwamba sheria hiyo inaashiria mwisho wa Hong Kong iliyokuwa ikifahamika ulimwenguni.
Marekani, Uingereza, Umoja wa Ulaya na Baraza la Haki za Binaadamu zimeelezea wasiwasi wao kuwa sheria hiyo itatumika kuwanyamazisha wakosoaji wa utawala wa China.