Kinondoni yapongezwa kwa kujenga uwanja wa mpira wa kisasa


Manispaa ya Kinondoni imepongezwa kwa ujenzi wa uwanja wa kisasa wa mpira wa miguu wenye uwezo wa kuchukua takriban idadi ya mashabiki 3600 kwa mara moja.

Pongezi hizo zimetolewa na Naibu wa Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Josephat Kandege wakati wa ziara yake katika Halmashauri hiyo kushuhudia uwanja huo wa kisasa ukijengwa katika eneo la Mwenge kwa mapato ya ndani utakaogharimu kiasi cha shilingi Bilioni 2.2 hadi kukamilika kwake.

Amesema kuwa mradi huo utakapokamilika utawezesha timu ya mpira ya Manispaa hiyo (KMC FC) kupata faida kubwa na hivyo kujiendesha yenyewe kupitia mapato yatakayokusanywa katika uwanja,na kuzitaka  timu kubwa ambazo hadi sasa hazina viwanja kuiga mfano huo.

“Niwapongeze sana Kinondoni, kwakujenga uwanja huu, utakapomalizika najua faida yake ipo wazi kabisa, kwanza inapendezesha, lakini pia inaleta changamoto kwa Halmashauri nyingine na timu kubwa kuiga kwenu, kama timu ya Kinondoni inaweza kuwa na uwanja wa kisasa wao wanashindwa nini” amesema Mhe. Kandege.



Hata hivyo Mhe. Kandege ameipongeza timu ya KMC FC kwakuendelea kufanya vizuri katika michezo yake na kusema kuwa kwa mwenendo huo  hivi sasa  inanafasi kubwa ya kushiriki ligi kuu katika msimu ujao.