Korea Kaskazini imesema itasitisha njia zote za mawasiliano na Korea Kusini wakati ikiendeleza shinikizo dhidi ya jirani yake kwa kushindwa kuwazuia wanaharakati kusambaza mpakani vipeperushi vya kuipinga Korea Kaskazini.
Shirika la habari la Korea Kaskazini limesema leo kuwa njia zote za mawasiliano ya pande mbili za mpakani zitasitishwa leo mchana.
Onyo hilo la Korea Kaskazini limekuja wakati mahusiano kati ya Korea hizo mbili yakiwa katika hali tete kutokana na mkwamo wa muda mrefu wa diplomasia ya nyuklia kati ya Korea Kaskazini na Marekani.
Baadhi ya watalaamu wanasema huenda Korea Kaskazini inatengeneza makusudi mazingira ya mvutano ili kuimarisha umoja wake ndani ya nchi au kuzusha uchochezi mkubwa kutokana na kuongezeka kwa vikwazo vya Marekani.
