Nyota watano wa Barcelona wakutwa na corona

Wakati Barcelona ikielekea kutimiza mwezi mmoja tangu iliporejea mazoezini kujiandaa na kurejea kwa ligi ya Hispania, imebainika kuwa nyota watano wa kikosi chake na makocha wawili waliambukizwa virusi vya Corona.

Taarifa hiyo imefichuliwa na kituo cha redio cha Cataran ambacho kimedai kuwa mastaa hao walipata maambukizi ya virusi hivyo vinavyo sababisha ugonjwa wa Covid19.

Hata hivyo, kituo hicho kimedai kuwa uongozi wa #Barcelona haukutaka kuweka hadharani majina ya nyota hao watano na makocha wawili waliopata maambukizi hayo na ilifanya siri kubwa kwenye jambo hilo hadi wahusika walivyo pimwa kwa mara ya pili na kuonekana hawana tena maambukizi.

Inadaiwa kuwa wachezaji hao hawakuonyesha dalili zozote za maambukizi ya virusi hivyo hadi pale walipopimwa na kubainika navyo.

Aidha, Ligi Kuu ya Hispania imepangwa kurejea tena Juni 11 kwa mchezo baina ya Real Betis na Sevilla. #Barcelona yenyewe itashuka uwanjani siku ya Juni 13 ikiwa ugenini dhidi ya Real Mallorca.