Umoja wa Ulaya waitolea mwito China kuruhusu kumbukumbu ya Tiananmen

Umoja wa Ulaya umesema licha ya wasiwasi wa kiafya kutokana na janga la ugonjwa wa Covid-19, China inapaswa kuwaruhusu watu wa HongKong na Macau kuadhimisha kumbukumbu ya umwagikaji wa damu uliotokea mwaka 1989 katika uwanja wa Tiananmen kufuatia ukandamizaji dhidi ya waandamanaji wakutetea demokrasia mjini Beijing.

Msemaji wa Umoja wa Ulaya ameuambia mkutano wa waandishi habari kwamba maadhimisho hayo ni ishara kwamba uhuru muhimu unaendelea kulindwa.

Kesho alhamisi ni siku ya maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 31 tangu wanajeshi wa China kufyetua risasi dhidi ya maandamano yaliyoongozwa na wanafunzi ndani na nje ya uwanja huo maarufu wa Tiananmen.