Awesu ashangazwa na kadi nyekundu aliyopewa na mwamuzi

KIUNGO wa Klabu ya Kagera Sugar, Awesu Awesu amesema kuwa hajui sababu ya kupewa kadi ya pili ya njano iliyomfanya atolewe nje jumla kwenye mchezo huo kwa kadi nyekundu.

Yanga jana iliikaribiisha Kagera Sugar kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho hatua ya robo fainali ambapo Kagera Sugar ilipoteza kwa kufungwa mabao 2-1.

Bao pekee la Kagera Sugar lilifungwa na Awesu Awesu dakika ya 19 huku yale ya yanga yakijazwa kimiani na David Molinga dakika ya 52 na lille la ushindi likipachikwa kimiani na Deus Kaseke kwa mkwaju wa penalti.

Awesu alionyeshwa kadi mbili za njano jambo lililofanya aonyeshhwe kadi nyekundu na mwamuzi wa kati jambo ambalo amesema kuwa hatambui sababu ya yeye kuonyeshwa kadi hizo.

Awesu amesema:"Sikuongea jambo lolote kadi ya kwanza nikishangaa namna nilivyopewa nikasema sawa, kadi ya pili nilikuwa nimechezewa faulo nikawa namtoa mchezaji mwenzangu maana nilishajua amepanic nashangaa nakutana na kadi nyingine sijui ilikuaje, sijaongea jambo lolote na wala sijatukana aulizwe hata refa mwenyewe.

"Niliyatarajia kwa kuwa tunacheza na timu kubwa na kongwe ambazo zina maagizo, hivyo kufungwa sijashangaa ni jambo la kawaida, ninachoumia ni kwamba nimeigharimu timu na bado tuna mechi za kucheza".

Msimu uliopita wa mwaka 2019, Kagera Sugar ilikwamia hatua ya robo fainali kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho na msimu huu imekwamia pia hatua ya robo fainali.