https://monetag.com/?ref_id=TTIb Kwa mara nyingine Marekani yala mweleka, UN yaunga mkono kwa kauli moja JCPOA | Muungwana BLOG

Kwa mara nyingine Marekani yala mweleka, UN yaunga mkono kwa kauli moja JCPOA


Balozi wa Iran nchini Uingereza amesema kuwa, kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kimeonesha mshikamano thabiti baina ya wanachama wake wote ukitoa Marekani. Wanachama wa baraza hilo wameunga mkono kikamilifu makubaliano ya nyuklia ya Iran yanayojulikana kwa jina maarufu la JCPOA na wamelaani siasa za kibeberu za Marekani.

Shirika la habari la IRNA limemnukuu Hamid Baeidinejad akisema hayo jana jioni katika ujumbe wake kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter na kuongeza kwamba, Marekani imetengwa vibaya na waitifaki wake kiasi kwamba waziri wa mambo ya nje wa nchi hiyo Mike Pompeo amelazimika kuondoka haraka (na kwa hasira) kwenye kikao hicho kabla hakijamalizika.

Jana Jumanne, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa liliitisha kikao cha kujadili ripoti ya tisa ya Katibu Mkuu wa umoja huo kuhusu utekelezaji wa azimio nambari 2231 lililopasisha makubaliano ya kimataifa ya nyuklia ya JCPOA.

Kikao hicho kimefanyika mjini New York Marekani kwa njia ya Intaneti kutokana na kuenea maambukizo ya kirusi cha corona na kupigwa marufuku mikusanyiko ya watu. Ajenda kuu ya kikao hicho ilikuwa ni kujadili ripoti hiyo ya tisa ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya utekelezaji wa azimio nambari 2231.

Katika kikao hicho waziri wa mambo ya nje wa Marekani amedai kuwa, kumalizika marufuku ya silaha kwa Iran, eti ni tishio kwa usalama na amani ya kimataifa.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Dk Mohammad Javad Zarif  amezungumzia chuki za Marekani kwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kusema kuwa, jamii ya kimataifa hasa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ilibidi muda mrefu nyuma iilazimishe Marekani itoe majibu kutokana na vitendo vyake viovu kama vile kuanzisha kwake ugaidi wa kiuchumi na kimatibabu dhidi ya wananchi wa Iran.