F Mtoto Azaliwa Bila Mikono na Miguu Babati, Afariki Baada ya Siku Mbili. | Muungwana BLOG

Mtoto Azaliwa Bila Mikono na Miguu Babati, Afariki Baada ya Siku Mbili.

 


Na John Walter-Babati

Katika hali isiyo ya kawaida, mama mmoja mkazi wa Kijiji cha Diffir, Kata ya Ufana, Wilaya ya Babati mkoani Manyara, amejifungua mtoto wa kiume bila mikono wala miguu katika Kituo cha Afya Bashnet.

Mtoto huyo alizaliwa Februari 9, 2026 siku ya Jumatatu majira ya saa tano usiku kwa njia ya kawaida, akiwa na uzito wa kilo 2.3.

Kwa mujibu wa Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Babati, Dkt. Madama Hosea, licha ya kuzaliwa bila viungo hivyo, mtoto alikuwa mzima na hakuwa na changamoto nyingine za kimaumbile wakati wa kuzaliwa.

Mtoto huyo alikuwa ni uzao wa 12 katika familia hiyo, ambapo wa kike ni wanne na wa kiume ni wanane akiwemo yeye.

Mama wa mtoto huyo ana umri wa miaka 47 na hakuwa mtumiaji wa pombe wala sigara wakati wa ujauzito.

Dkt. Madama, aliyeongoza timu ya wataalamu wa afya kufika katika kituo hicho kufuatilia tukio hilo, alisema kuwa katika kipindi chake cha miaka 15 ya utumishi kama daktari hajawahi kukutana na tukio la aina hiyo.

Aidha, alieleza kuwa matumizi ya pombe na tumbaku kwa mama mjamzito, hasa katika miezi mitatu ya mwanzo wa ujauzito, yanaweza kusababisha changamoto za kimaumbile kwa mtoto. Hata hivyo, katika tukio hili, mama huyo hakuwa na historia ya matumizi ya vitu hivyo.

Kwa masikitiko, mtoto huyo alifariki dunia Februari 11, 2026 siku ya Jumatano majira ya saa tano usiku, baada ya kupata degedege kali.

Awali mama alionekana kutaharuki, lakini yeye na mume wake walikubali hali hiyo kwa moyo wa subira.

Amesema kuwa kama mtoto wao asingefariki, wangemlea kama mtoto mwingine yeyote.

Dkt. Madama ametoa wito kwa kina mama wajawazito kuhakikisha wanahudhuria kliniki zote nane kama inavyoshauriwa na wataalamu wa afya, pamoja na kutumia dawa za madini ya chuma na virutubisho vingine wanavyopewa ili kulinda afya zao na za watoto wao.

Ameongeza kuwa Kituo cha Afya Bashnet, kilichojengwa kwa mapato ya ndani kwa gharama ya zaidi ya shilingi milioni 600, kimeendelea kuwa mkombozi mkubwa wa huduma za afya katika Kanda ya Bashnet na maeneo ya jirani.

Licha ya changamoto hiyo, familia imesema mtoto huyo alikuwa ni zawadi kutoka kwa Mungu, na wamepokea yote yaliyotokea kwa imani na utulivu.


Chapisha Maoni

0 Maoni