Zoezi la uchukuaji fomu ya kuwania Urais, Ubunge na uwakilishi CHADEMA kuanza leo

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo( CHADEMA)kimekukumbusha kuwa ratiba ya shughuli ya uchukuaji, kutafuta wadhamini na kurejesha fomu za kugombea nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Urais wa Zanzibar, Ubunge na  Uwakilishi linaanza rasmi leo.

Taarifa iliyotolewa leo na Chadema kupitia kitengo chake cha mawasiliano kimesema kwamba watia nia nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania watachukua fomu zao za kugombea Ofisi za Makao Makuu ya Chama, Mtaa wa Ufipa, Kinondoni, jijini Dar es Salaam.

Wakati kwa upande wa Watia nia wa Urais wa Zanzibar watachukua fomu zao Makao Makuu ya Chama, Kisiwandui, Unguja, Zanzibar.

"Leo Jumamosi, Julai 4, 2020, saa nne asubuhi wapo watia nia watachukua fomu. Vyombo vya habari vinakaribishwa katika shughuli hiyo na vinaombwa kufika kwa wakati,"imesema taarifa hiyo.

Wakati huo huo baadae leo hii hii kuanzia saa 5.30, Katibu Mkuu wa Chama John Mnyika atakuwa na kikao na watia nia wa ubunge na udiwani wa Kanda ya Pwani, itakayofanyika Hoteli ya Lions, Sinza, jijini Dar es Salaam.