Mwanamke, jambo hili ni muhimu sana katika mahusiano yako

Kama umeolewa wewe, umechaguliwa wewe ndiyo mpenzi wake hebu acha kushindana na watu wengine, acha kushindana na X wake au wanawake wengine ambao unadhani kuwa wanamtaka mume wako. Nilazima ujue kuwa mume wako alikuwa na watu kabla yako lakini pia kuna watu bado wanamtaka na hawatajali kama ameoa au hajaoa.

Lakini yeye hajawachagua wao kakuchagua wewe, iwe ni kwamba ulimtegeshea mimba, ulienda kwa mganga au alilazimishwa na wazazi wake lakini mwisho wa siku ni kuwa yuko na wewe na hao wengine kuna kitu umewazidi hivyo huna haja ya kushindana nao tena. Umeshashinda kazi unachotakiwa kufanya ni kuulinda ushindi wako na si kushindana na wengine.

Kuhangaika kutukanana nao, kuhangaika kuvaa kama wao, kuhangaika kuwafuatilia maisha yao kunakupa hasara kuu mbili.

Kwanza ni kuwa unakuwa huishi maisha yako, unakuwa huna furaha na kazi yako kubwa ni kujilinganisha, kwamba badala ya kufurahia ndoa wewe kazi ni kuangalia wamevaa nini, wanaishije, wana nini hivyo unakuwa huna amani na huna furaha.

Pili ni kuwa unakuwa kero kwa mume wako unachosha, kwamba kama kila siku unakuwa unamuuliza mbona ulikuwa na fulani, nilikuona unaongea na fulani, fulani hivi fulani vile. Huna furaha una kisirani kila siku, unamfanya mwanaume kujiuliza hivi kweli nilifanya uchaguzi sahihi kumuoa huyu mwanamke. Si bora hata ningemuoa fulani labda ningekuwa na amani.

Unamlazimisha mume wako kuenda kutafuta amani huko kwingine, kama mwanaume kila siku akirudi nyumbani hamuwezi kuongea kitu cha maana zaidi ya kukagua simu yake, kuulizia alikuwa wapi na na nani, kumzungumzia X wake basi atatafuta sehemu ya kupumzisha kichwa. Yaani mtu ofisini akutane na kero za bosi au wateja na akirudi nyumbani anakutana na kero za mke ambaye amemuoa, atachepuka tu hamna namna!

Sisemi uvumilie kama mume wako anachepuka au anafanya ujinga huko nje hapana, lakini kama hajakuonyesha dalili yoyote ya kuchepuka, kama hajaonyesha hata kama anawataka hao watu unaowawaza, hebu acha kisirani eti kisa kaongea nao. Mwanaume awezi kuacha kuongea na mtu fulani eti kisa hujiamini na unadhani atakusaliti nao!

Kwanza kama kweli ni mchepukaji mzuri watu anaochepuka nao hata namba za simu zao huwezi kukuta katika simu yake. Hata siku moja huwezi kukuta anaongea nao hivyo kwanini ujipe presha na vitu ambavyo vipo kichwani kwako tu. Acha kuharibu ndoa yako na kama hujui nini cha kufanya basi jifunze jinsi ya kujipa furaha yako. inawezekana unahisi unasalitiwa kumbe unamlazimisha mume wako kukusaliti.