Waliokaidi wito wa Takukuru kusakwa popote walipo


Na John Walter-Babati


Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Manyara imetangaza msako mkali kwa wanachama wa Babati Sacco's  waliokaidi kuripoti katika Ofisi za Takukuru kama walivyotakiwa.


Taarifa iliyotolewa Leo Jumatano Agosti 12,2020 na Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Manyara Holle Makungu, imeeleza kuwa wamefikia uamuzi huo  baada ya baadhi ya wanachama waliochukua Fedha za Saccos hiyo na muda wa kurejesha kupita, kukaidi kufika kwa hiari kwenye ofisi za Takukuru mjini Babati Agosti 10 ili wapewe hesabu zao.


Makungu amesema wengi wao wameonyesha uungwana  kama walivyoelekeza na tayari wamewapa hesabu zao na kuanza  kurejesha fedha hizo.


Amewataja waliogoma kufika ni wanachama tisa ambao  ni Halima Chacha,Akida Mzamba,Athuman  Kavumo,Simon Alawa,Stela Mariki,Frida  John,Hamadi Hoti,Elisante Palangyo na Anjela Sure.


Makungu amesema watu hao wataanza kusakwa popote walipo kuanzia kesho Agosti 13, na kufikishwa kwenye mikono ya Sheria na kufunguliwa Mashtaka kwa makosa ya kula njama na kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu.


Aidha taarifa imeeleza kuwa wanaendelea kuwashikikilia  wanachama wawili Yuda Sendeu na Kusirie Urasa  kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria.

Post a Comment

0 Comments