Na Omary Mngindo, Nianjema - Sept 11
VIJANA wapatao 1,500 wanaoishi ndani ya Jimbo la Bagamoyo Mkoa wa Pwani, wanataraji kunufaika na ajira katika viwanda mbalimbali vilivyopo jimboni hapa.

Hatua hiyo inayolenga kuboresha hali ya kiuchumi kwa walengwa hao atika viwanda hivyo, pia itaongeza mzunguko wa fedha kupitia malipo watayokuwa wanayapata hatua inayofuatia dhamira ya Serikali chini ya Rais Dkt. John Magufuli.

Hayo yamebainishwa na mgombea Ubunge jimboni hapa Muharami Mkenge, akizungumza na wakazi waishio ndani ya Kata hiyo, katika mkutano uliofanyika shule ya msingi Nianjema, ambapo alisema kwa sasa wakati kilimo cha miwa na ujenzi ukiendelea vijana 600 wanafanya kazi mbalimbali.

"Ndugu zangu wana-Nianjema niwaombe ifikapo Oktoba 11 tuamke mapema tukapige kura kishindo kwa kuwachagua Rais Dkt. John Magufuli, mbunge Muharami Mkenge pamoja na diwani Abdul Pyalla ili kwa umoja wetu tukamalizie mazuri tuliyoyaanza," alisema Mkenge.

Kwa upande wake Meneja wa Kampeni Yahya Msonde aliwaambia wananchi hao kuwa, wakati Serikali ya awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli inaingia madarakani mwaka 2015, makusanyo ya Serikali kwa mwezi kulikuwa shilingi bilioni 850, sasa yamefikia tririoni 1.3 kwa mwezi.

"Ndugu zangu kwa juhudi hizi peke yake ukiachia shughuli mbalimbali zinazofanywa na serikali yetu chini ya Jemedali wetu Dkt. John Magufuli, ni kielelezo tosha kwamba anafaa kuchaguliwa tena, ili kazi aliyoianza aweze kuiendeleza," alisema Msonde.

Mgombea udiwani katani humo Abdul Pyalla alisema kuwa, katika kipindi cha miaka mitano inayoishia kwa kushirikiana na wananchi, viongozi wenzake na halmashauri kazi mbalimbali za kimaendeleo zimefanyika, huku akiushukuru uongozi wa Mamlaka ya Mawasiliano TCRA kwa msaada walioipatia Kata yake.

"Kwa ushirikiano na Serikali yetu kupitia Halmashauri, wadau wa maendeleo na wana-Nianjema tumejenga zahanati, tumeongeza madarasa, matundu ya vyoo pamoja na ujenzi wa ofisi ya Kata ambazo wakati wowote zitafunguliwa," alisema Pyalla.