F TBS atoa elimu kwa wazalishaji, Wasambazaji na Wauzaji wa mafuta ya kula | Muungwana BLOG
https://c2p.cleverwebserver.com/dashboard/6a0bec4b-79ba-11ef-ad2b-06f0639468d1

TBS atoa elimu kwa wazalishaji, Wasambazaji na Wauzaji wa mafuta ya kula

 


SERIKALI imesema ipo kwenye mchakato wa kuongeza uzalishaji  wa mafuta ya kula nchini kwa mazao yote yanayotoa mafuta  ikiwemo alizeti, na michikichi  ili kupunguza gharama za kuingiza mafuta kutoka nje ya nchi.

Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dodoma na Mkurugenzi wa udhibiti ubora {TBS} Bw.Lazaro  Msasalaga wakati akitoa mafunzo kwenye semina kwa wazalishaji,wasambazaji,na wauzaji wa mafuta ya kula.


Mafunzo haya yamelenga kuwaelimisha wadau hao juu ya uzalishaji bora, uhifadhi sahihi wa bidhaa za mafuta haswa sehemu za kuuzia, ufungashaji sahihi na salama na umuhimu wa kuzingatia na kuweka taarifa sahihi na muhimu katika vifungashio.

Amesema lengo kubwa la serikali  ni kuzingatia mahitaji makubwa ambayo kwa sasa  wananchi wanahitaji ili kuweza kuzalisha mafuta ya kula kwa wingi nchini.

“Waziri ana mradi mkubwa wa  kupanda michikichi kule Kigoma lengo kubwa ni kuongeza uzalishaji wa mafuta nchini, na si kwenye michikichi tu inaenda kuangalia na uzalishaji wa mazao mengine kama alizeti na namna Mkoa husika unavyoweza kuzalisha zao hilo“ amesema Msasalaga

Aidha amesema  katika mafunzo hayo  wamepita wilaya zote  za mkoa wa Dodoma, Singida na Tabora ili kuweza kuwaelimisha wazalishaji na wauzaji namna ya kuyatunza mafuta ili  yawe na ubora.

“ Tumeenda Kongwa Kibaigwa,Mpwapwa, Chamwino, Kondoa, na wengine wapo mikoa ya Singida na Tabora, tukitoka Dodoma jiji tutamalizia Bahi, Manyoni na Itigi kuendelea kusambaza elimu hii japo Kuna changamoto ambazo tunazipata lakini nasi tunaziwekea mikakati  kiukweli kama mafuta yasipofungashwa vizuri kwa kupigwa na mwanga wa jua mafuta yanaweza kuharibika”

 Amesema katika mafunzo hayo wanasisitiza katika uhifadhi ndio maana wamewatembelea  wauzaji wa barabarani waweke vibanda kukinga mafuta   kwani jua linapopiga mafuta yanaharibika.

Msasalaga ametoa ushauri kwa wadau hao kuzingatia kanuni za uzalishaji na uhifadhi bora na salama ili kuepuka kupoteza masoko na kero ya kukutwa na bidhaa hafifu ambayo itawalazimu kuteketeza kwa gharama zao.

 


Naye Daudi  Makala, Mzalishaji mdogo wa mafuta ya alizeti amesema  kuwa wamejifunza namna ya kuzingatia ubora wa mafuta  kwani kwa kufanya hivyo  atampa uhakika mtumiaji .

“ Pia tuhakikishe mbegu  imekomaa na usafi pamoja na utayalishaji wa mafuta haya kiukweli tumejifunza mambo mengi tukizingatia nafikiri walaji watafurahia  ,sisi wasindikaji wa mafuta inabidi sasa mara kwa mara tuwe na semina  ili tuweze kukumbushana “ amesema Makala

 Muuzaji  kutoka soko la saba saba Bi.Eunice Maneno amesema kuwa  kutokana na semina  amejifunza mambo mengi kutoka kwa mkulima hadi kufikia mafuta yenyewe .

“ Wakati mwingine unaweza kununua mafuta machungu  kumbe ni kutokana na  mkulima kukimbilia soko anaweza akakamua mafuta ambayo mbegu  haijakauka kwahyo mi niombe tu semina hizi tuzipate mara kwa mara na niwaombe wananchi watumie mafuta haya ya alizeti kwani ni mazuri kwa afya”.Amesema Eunice.

Mpaka sasa wadau zaidi ya 400 kutoka Kongwa, Chamwino, Mpwapwa, Kibaigwa,Kondoa na Dodoma Mjini wamefikiwa na mafunzo haya, ambapo maeneo ya Bahi watafikiwa kesho tarehe 29.09.2020.

Post a Comment

0 Comments