WHO kuweka kanuni za kupima dawa za mitishamba za Afrika

 


Shirika la afya duniani (WHO) limekubali kanuni za kupima dawa za mitishamba za Afrika kwa ajili ya mapambano dhidi ya Covid-19.


Sayansi itakuwa ndio msingi wa vipimo hivyo kwa ajili ya usalama na ufanisi wa dawa ambazo zitaidhinishwa,imesema WHO.


Madawa yoyote ya kienyeji ambayo yanaaminika kuwa yana ufanisi yanaweza kuharakishwa kutengenezwa kwa kiango kikubwa.


Rais wa Madagascar amekuwa akinadi dawa ya asili ambayo haijafanyiwa vipimo ambayo anasema inaweza kutibu virusi vya corona, licha ya onyo la WHO dhidi ya matumizi ya dawa hizo za mitishamba.


WHO ilisema kuwa kanuni mpya zinalenga kusaidia na kuwawezesha wanasayansi wa Afrika kufanya majaribio yanayofaa ya kimatibabu.


Hatua hiyo inakuja baada ya idadi ya wagonjwa waliothibitishwa duniani kupita milioni 30, huku vifo vyote vilivyothibitishwa duniani vikiwa zaidi ya 957,000. Barani Afrika zaidi ya watu milioni 1.3 wamepatwa na maambukizi ya corona na zaidi ya vifo 33,000 vimeripotiwa.


Chanjo 140 zenye uwezekano wa kuwa chanjo kamili ya Covid-19 zinatengenezwa kote duniani , huku makumi kadhaa ya chanjo hizo zikiwa tayari zinafayiwa vipimo katika kliniki za majaribio ya chanjo.


'Kuharakishwa kwa utafiti'

Sambamba na juhudi hizi, kliniki za majaribio ya awamu ya tatu zimepewa ruhusa ya kuendelea kutumia dawa za kiasili za Afrika.


Jopo la wataalamu, linalojumuisha WHO, Kituo chakudhibiti na kuzuwia magonjwa cha Muungano wa Afrika na tume ya Muungano wa Afrika ya masuala ya kijamii, wamekubaliana juu ya mpangilio wa shughuli hiyo.


Awamu ya tatu ya majaribio kwa kawaida hupima usalama na ufanisi wa dawa kwa kundi kubwa la watu wanaoshiriki.


"Kuidhinishwa kwa nyaraka za kiufundi kutahakikisha kwamba ushahidi wa pamoja wa kimatibabu wa ufanisi wa dawa hizo asili kwa ajili ya tiba ya Covid-19 unapatikana bila kukiuka usalama wake ," amesema Profesa Motlalepula Gilbert Matsabisa, mwenyekiti wa jopo hilo la wataalamu

Post a Comment

0 Comments