Zitambue faida 10 za Kuwa na Malengo Maishani

 

Kabla hujakamilisha chochote maishani, ni lazima ufahamu unahitaji nini. Ni lazima ukae chini utafakari kama kile unachokifanya kina thamani kwako; ikiwa hakina thamani, basi tenga muda ujiwekee malengo yenye maana kwako.

“Maisha bila malengo ni sawa na kuanza safari bila kufahamu unakotaka kwenda au kufika.”

Kujiwekea malengo maishani kuna umuhimu mkubwa kwani hutufanya tujikite sawasawa kwenye kila tunachokifanya.

“Kujiwekea malengo ni hatua ya kwanza ya kufanya visivyoonekana vionekane”

Tony Robbins
Je uko tayari kuweka malengo? Karibu nikufahamishe faida 10 utakazozipata ikiwa utajiwekea malengo maishani mwako.

1. Hukupa mwongozo
Awali ya yote, malengo hukupa mwongozo na mwelekeo maishani mwako. Malengo hukuwezesha kubaini kitu unachokilenga, na hukufanya uelekeze nguvu zako kwenye kitu husika.

Badala ya kushika hiki na kile au kuwa huyu na yule, malengo yatakuwezesha kufahamu unatakiwa kufanya nini au kuwa nani.

2. Hukuwezesha kufanya maamuzi
Baada ya kujiwekea malengo utaweza kubaini ni maamuzi gani yanafaa na ni yapi hayafai kulingana na malengo uliyojiwekea.

Pia utaweza kufahamu mambo ya msingi maishani mwako, hivyo utaweza kufanya maamuzi kulingana na mambo hayo.

Mtu mwenye malengo huwa makini kwenye maamuzi yake kwani analinda asije akafanya maamuzi yatakayoathiri lengo lake.

3. Hukuwezesha kutawala baadaye yako
Unapokuwa na malengo na mipango stahiki ya kuyatimiza, ni wazi kuwa moja kwa moja umeshatawala baadaye yako.

Kuweka malengo ni jambo zuri ambalo litakuwezesha kufahamu aina na mfumo wa maisha yako ya baadaye. Jambo muhimu ni kuhakikisha kuwa unaweka mipango sahihi na inayotekelezeka ya kutimiza malengo yako.

Ni muhimu kuhakikisha kila siku kuna kitu kinachofanyika ili kukamilisha sehemu fulani ya malengo uliyojiwekea maishani.

“Malengo ni ramani ya barabara inayokuongoza na kukuonyesha ni nini kinawezekana kwenye maisha yako”

Les Brown

4. Hukuwezesha kujikita kwenye mambo muhimu
Kuna mambo mengi kwenye maisha yetu ya kilasiku, lakini siyo yote ni ya muhimu kwenye kutimiza ndoto zetu.

Ukiwa na malengo ni rahisi kubaini mipango au mambo yasiyokuwa na umuhimu kwa kutazama yale yote yanayokinzana na malengo yako.

Haijalishi unalipenda jambo fulani kwa kiasi gani, kama linakinzana na malengo yako, basi huna budi kuliacha.

5. Malengo hukuhamasisha
Unapotazama uzuri na ubora wa malengo yako unapata matumaini na hamasa kubwa.

Hamasa huzidi pale ambapo unaanza kuona ukikamilisha malengo yako ya muda mfupi; hili hukuhamasisha kufanya bidii zaidi ili kuyafikia yale ya muda mrefu.

Ni wazi kuwa chanzo kizuri cha hamasa, ni kujiwekea malengo na kuanza kuyatimiza.

“Jenga ndoto zako wewe mwenyewe, la sivyo mtu mwingine atakuajiri kujenga zake.”

Farrah Gray


6. Hutusaidia tusipoteze muda
Mtu mwenye malengo kamwe hawezi kupoteza muda. Ukiwa una malengo ni wazi kuwa muda wako wote utakuwa umegawanywa kwenye kuyafanyia kazi na kuyatimiza malengo yako.

Kwa njia ya kujiwekea malengo hutopoteza muda kwa kufanya mambo ambayo hayakuwezeshi kufikia ndoto na malengo yako.

Haitarajiwi mtu mwenye malengo kuwa mlevi, mvivu, anayechelewa kuamka, anayeshinda kwenye mitandao ya kijamii au vijiwe n.k.

7. Hukuwezesha kufanya uwekezaji sahihi
Ukiwa na malengo ni wazi kuwa utafahamu nini, wapi na lini uwekeze; kwani malengo yako yatakuwezesha kubaini ni uwekezaji gani unaoendana na lengo lako.

Lakini usipokuwa na malengo utawekeza kwenye kila kitu kinachokuja mbele yako na matokeo yake hutoweza kufanikiwa.

8. Malengo hukuwezesha kujitathimini
Unapimaje kufanikiwa kwako kama huna kipimo cha kupimia kufanikiwa huko? Malengo ni kipimo muhimu kitakachokuwezesha kutathimini kama umefanikiwa au la.

Ukiwa na malengo ni rahisi kutazama kama yale uliyoyafanya au unayoyafanya yamekuwezesha kutimiza au kufikia lengo lako.

Ikiwa yamekuwezesha, basi unafanya vizuri; lakini ikiwa hayajakuwezesha kufikia lengo, basi kuna mambo ya kuyatazama upya.

9. Hukufanya upende kile unachokifanya
Kama nilivyotangulia kusema pale awali, kuwa malengo hukuongoza kufahamu unatakiwa kufanya nini, malengo pia yatakuwezesha upende kile unachokifanya.

Ni ukweli usiopingika kuwa ukifanya kitu ambacho unajua kinakamilisha malengo yako utakipenda. Hivyo ni muhimu kuwa na malengo ili yatufanye tupende kile tunachokifanya.

Kwa mfano ukiwa na lengo la kupata kipato cha Sh. 7,000,000 kwa mwezi, ni wazi kuwa utapenda kile unachokifanya kwani kinakuwezesha kutimiza lengo lako.

10. Ujasiri binafsi
Watu wenye malengo wana ujasiri binafsi mkubwa, wanaamini wao siyo kama watu wengine kwa sababu kuna vitu wanavyoviona tofauti na watu wengine.

Mtu mwenye malengo anajiamini kuhusu maisha yake ya sasa na ya baadaye kwa sababu ana mipango na mikakati stahiki katika maisha yake.

Neno la mwisho:

Kumbuka “mpango mzuri leo ni bora kuliko mpango mkamilifu kesho.” Naamini umefahamu wazi umuhimu wa kujiwekea malengo maishani mwako. Je wewe una malengo? Je unafanya kazi kuyatimiza?

Post a Comment

0 Comments