Kanuni sita za ufugaji bora wa kuku wa kienyeji


Kuku wa kienyeji ni wazuri kwa ufugaji kwa sababu: Wanavumilia sana magonjwa, Ni rahisi kuwahudumia, Chakula chao ni cha bei ya chini, Wavumilivu wa hali tofauti za hewa, Hawahitaji uangalizi wa karibu, na soko lake ni kubwa sana na bei nzuri). Hii haimaanishi kwamba, uwaache kuku bila uangalizi, kwani nao hupata magonjwa kama wasipo patiwa chanjo sahihi, hupungua uzito na uzalishaji mayai hushuka kama wasipo patiwa chakula chenye virutubisho vyote. Hapa naelezea vitu muhimu katika hii formula ya ufugaji kuku wa kienyeji kwa mafanikio:

1. Aina ya kuku: Chagua aina ya kuku wenye uwezo wa kutaga mayai mengi na wakati huohuo, kuzalisha nyama nyingi. Hii itakupa faida kote, kwenye upande wa nyama na upande wa mayai. Kuku hawa wanajulikana kama Chotara, wanatabia sawa na kuku wa kienyeji wenye asili ya Tanzania wanaopatikana maeneo mengi nchini; kutokana na uvumilivu wao wa magonjwa na hali tofauti za mazingira. Pia wanauwezo wa kutaga mayai mengi (Wastani wa mayai matano kwa wiki) karibu sawa na kuku wa kizungu. Aina ya kuku hawa ni kama vile, Chotara wekundu (Rhode Island Red), Black Australorp (Weusi/Malawi), Barred Plymouth Rocks (Madoa), New Hamshire Red, Kuroila wanapatikana sana Uganda, na Kari kutoka Kenya. Hizi ni aina ya kuku zinazo patikana Tanzania.

2. Chanjo: Kama nilivyosema mwanzo, kuku wa kienyeji ni wavumilivu wa magonjwa lakini si kwamba hawayapati, kuna magonjwa ambayo ni hatari pia kwa kuku wa kienyeji. Chanjo ni muhimu kuwaepusha na hatari ya kuyapata magonjwa haya. Chanjo muhimu kwa kuku wa kienyeji ni; New Castle, Gumboro, Marek’s na Ndui ya kuku. Fuata utaratibu wa chanjo kutokana na ushauri wa daktari. 

3. Chakula: Kuku wa kienyeji pia wanahitaji mchanganyiko sahihi wa chakula, ili waweze kukupatia mazao mengi na bora, na kuwaepusha na magonjwa. Zipo fomula mbalimbali za chakula kutokana na umri wa kuku, na aina ya kuku. Kuku wote wanahitaji chakula chenye mchanganyiko sahihi wa Madini, Vitamini, Protini, Fats, Wanga, Vyakula vya kulinda mwili ili usipatwe na maradhi, na Maji safi. Muhimu kuwapatia kuku majani kama ziada ya chakula, hii hupunguza gharama za chakula na kuwafanya kuku waonekane wenye afya bora. Ni vizuri kuwapatia vifaranga chakula spesheli cha dukani kama huna ujuzi wa kutengeneza mwenyewe. Kwani vifaranga wengi hufa kutokana na kutokupata chakula chenye mchanganyiko sahihi kwao. Kuku wa mayai pia wanahitaji mchanganyiko sahihi ili waweze kutaga mayai kwa wingi.

4. Banda: Kuku wa kienyeji pia, wanahitaji banda au nyumba ya kuku imara ili kuweza kuwakinga na baridi kali, wanyama hatari, na wizi. Banda pia liwe na sehemu nzuri za kutagia na sehemu za kulala ziwe juu , kwani kuku hupendelea kulala juu. Ni muhimu banda liwe katika hali ya usafi muda wote. Kwa hivyo ni vizuri linyanyuliwe juu kidogo ili kuruhusu uchafu kuanguka chini na lijengwe ka kutumia mbao, mabanzi, milunda, nyavu, na mabati. Vifaranga wanahitaji kutenganishwa na kuku wakubwa. Banda si lazima liwe la gharama kubwa, kwani mafanikio ya ufugaji wa kuku ni vile unavyo waangalia na si banda. Mada inayohusu mabanda bora ya kuku itakuja hivi karibuni.

5. Majogoo kwa majike: Ili mayai mengi yaweze kutotolewa, ni vizuri jogoo mmoja aweze kuwahudumia majike wasiozidi 7. Kwani kuku wanaweza kutaga bila ya jogoo, lakini mayai hayatoweza kuleta kifaranga. Ili mayai yalete vifaranga ni lazima yawe yamerutubishwa (Fertilized eggs) na jogoo. Kwa hivyo ni vizuri kuweka Jogoo 1 kwa majike 7, hivyohivyo Jogoo 2 majike 14, Jogoo 3 majike 21, n.k. Pia hakikisha kuku wanao tumika kuendeleza kizazi ni wale wenye afya bora. 

6. Vyombo vya chakula: Hakikisha vyombo vya chakula ni visafi na vinawatosheleza kuku wote. Vyombo hivi ni vizuri vifanyiwe usafi wa mara kwa mara, ili kuwaepusha kuku na magonjwa. Maji machafu huwa ni chanzo kikuu cha magonjwa hasa ya kuhara. Hakikisha kuku wako wanabadilishiwa maji angalau mara mbili kwa siku. 


Post a Comment

0 Comments