Na Amiri Kilagalila,Njombe
Mkulima na mtaalamu wa kilimo cha zao la Parachichi mkoani Njombe Bw,Obed Mgaya amekemea wakulima kutumia njia ya simu kulima zao hilo huku wakiwa mbali na mashamba yao,kwa lengo la kuboresha zao hilo ili kufikia malengo ya uchumi kupitia kilimo.
Mgaya ametoa onyo hilo wakati akitoa mafunzo kwa vitendo kwa wakulima zaidi ya 50 kutoka kata ya Matamba na Ikuwo wilayani Makete waliofika katika mashamba yake yaliyopo kijiji cha Igagala wilayani Wanging’ombe na kuwakumbusha umuhimu wa kutumia maafisa ugani waliopo katika maeneo yao huku akionya tabia ya baadhi ya wawekezaji katika zao hilo kutumia kilimo cha simu badala ya kufika mashambani.
“Matunda ni lazima uhakikishe unaboresha shamba na mpaka sasa hivi mimi ninakataa wanaosema haya matunda yatakuwa kama mikusu hapana! Haiwezekani na haiji kutokea,kwasababu wapo waboreshaji na wapo wasioboresha.wapo wanaolima kwa njia ya simu hawajafika hata shambani”alisema Mgaya
Ameongeza kuwa “Utakuta umeweka kibarua hapa harafu anakupigia simu uko Dar es Salaam Mzee! Shamba lako hili harafu unamrushia picha kumbe umepiga shamba la jirani”aliongeza Mgaya
Jofrey Augstino Ngogo ni katibu mkuu wa dayosisi ya kusini Magharibi wa kanisa la kinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) aliyeongozana na wakulima hao ameeleza dhima ya kujifunza kilimo hicho.
“Lengo letu ni maarifa namna ya kilimo cha parachichi kwasababu tumeanza na zoezi la kuwagawia miche,kwasababu sisi kama dayosisi tuanaamini katika jamii kuwa mhimili mkuu wa kuendesha mambo yanayohusu dayosisi,kwa hiyo kubwa zaidi ni kuwajengea uwezo na kuendesha kilimo cha parachichi chenye tija”alisema Ngogo
Mara baada ya kupata elimu baadhi ya wakulima akiwemo Elesia Nyato wakakiri kuwa kilimo cha parachichi kinahitaji elimu ya kutosha huku wakiwasihi akina mama kuwekeza katika kilimo hicho.
“Tujitahidi wamama katika kilimo hiki kwa kuwa parachichi inaokoa sana na ukipanda mwa huu,basi mwaka wa tatu unakuwa sokoni na mimi nina kama ekari mbili na miche niliyoanza kuchuma ni 57 nimeyatunza vizuri na mchumo wa kwanza nimechuma na kuuza na kufanikiwa kupata milioni 3”alisema Elesia Nyato
