Mahakama moja mjini Machakos nchini Kenya, imepitisha hukumu ya kifungo cha miaka 30 gerezani baada ya kupatikana na hatia kwa kosa la kumkata mke wake mikono yote miwili mwaka 2016.
Mikono miwili ya Jackline Mwende ilishambuliwa vibaya na mume wake na kukatwa kwa kutumia kisu kikubwa kwasababu ya kushindwa kumzalia watoto, katika kile kinasemekana ni kisa kibaya zaidi cha ugomvi wa nyumbani.
Kisa hicho kilitokea kijiji cha Kathama, eneo la Masii katika kaunti ya Machakos licha ya wawili hao kuwa kwenye ndoa kwa miaka saba.
Mikono ya Bi. Jackline Mwende ilikatwa kuanzia kwenye kifundo cha mkono na mumewe Stephen Ngila Thenge tarehe 24 mwezi Julai 2016.
Kando na kukatwa mikono, Jackline Mwende pia alipata majeraha mabaya kichwani na mgongoni.
Ndugu zake walisema kuwa wanandoa hao walikuwa na matatizo na kwamba Bi. Mwende alitaka kumwacha mumewe, lakini akashauriwa kutofanya hivyo na kiongozi mmoja wa dini.
''Sijui kwa nini alikuwa akinilaumu licha ya sisi sote kwenda hospitalini mwaka uliopita na kwamba daktari alisema kuwa ni yeye aliyekuwa na tatizo la kuzaa ambalo linaweza kurekebishwa'', Bi. Mwende alisema.
Wakati huo katika mahojiano na gazeti na Daily Nation, Mwende alisema kuwa hali hii ilichangia aanze uhusiano mwingine na ikaripotiwa kuwa ni mjamzito.
Bi. Jackline alisema alikuwa na haja ya kuwa na watoto ndipo akaanza uhusiano na mwanamume mwingine ili kuokoa ndoa yake, lakini mumewe ambaye sasa amefungwa jela, akagundua.
"Nilikuwa ninataka mtoto. Nilikuwa na haja ya mtoto...na pia ibilisi alisababisha mimi kutembea nje ya ndoa yangu. Haikuwa vizuri kufanya hivyo, ninajua watu watanihukumu vikali kwasababu ya hilo. Kwa vile niko hai na nitajifungua mtoto hivi karibuni, nina matumaini licha ya kupitia taabu'', Mwende alisema.
