Raia 41 wa Ethiopia wamekamatwa nchini Tanzania katika kijiji cha Kiruru wilayani Mwanga wakidaiwa kuingia nchini kinyume na sheria.
Kamanda wa uhamiaji Mkoa wa Kilimanjaro, Edward Mwenda akizungumza leo Jumatano Februari 3, 2021 amesema raia hao walitelekezwa na mwenyeji wao katika kijiji hicho kilichopo mpaka wa Tanzania na Kenya.
Amebainisha kuwa walikamatwa usiku wa kuamkia Jumatatu Februari mosi, 2021 katika kijiji hicho na cha Lembeni na walipoulizwa walidai wameingia nchini kupitia madalali na walikuwa na lengo la kwenda nchini Afrika Kusini kupitia Msumbiji.
“Tunatoa onyo kwa watu wote wanaojihusisha na biashara ya usafirishaji wa wahamiaji kwa sababu tunatambua nyendo na mbinu wanazotumia tutawakamata," amesema Mwenda.
