Mahakama ya hakimu mkazi Arusha leo Jumatano Februari 3, 2021 imeahirisha tena kutoa hukumu ya kesi ya kusafirisha dawa za kulevya inayomkabili mkazi wa jijini Arusha, Mkami Shirima.
Mkami pia anakabiliwa na kesi nyingine ya kumuua mfanyakazi wake wa ndani, Salome Zakaria(18).
Katika kesi hiyo hakimu mkazi, Gwantwa Mwankuga amesema Shirima anatuhumiwa kusafirisha dawa za kulevya aina ya Mirungi yenye uzito wa kilo 2.95 kinyume cha Sheria.
Mtuhumiwa huyo anadaiwa kutenda kosa hilo Septemba 24, 2019 katika eneo la Mianzini mkoani Arusha akiwa na mwenzake, Emaliana Laizer wakitaka kusafirisha kilo 2.9 za mirungi.
Hakimu huyo ameahirisha kusoma hukumu hiyo kutokana na kutokamilika huku Shirima akirejeshwa rumande.
