Waziri wa mambo ya nje wa Marekani kukutana na viongozi wa India


Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken leo atakutana na viongozi wa India akiwa katika ziara yake ya kwanza nchini humo kama mwanadiplomasia wa ngazi ya juu. 
 
Maafisa wa India wanatarajia kuzungumzia wasiwasi wao juu ya kujiimarisha kwa wanamgambo wa kundi la Taliban nchini Afghanistan pamoja na kuishinikiza Marekani kuiunga mkono zaidi India dhidi ya China. 
 
Kwa upande wake waziri huyo wa mambo ya nje wa Marekani anatarajiwa kuzungumzia wasiwasi uliopo juu ya haki za binadamu wakati atakapokutana na waziri mkuu wa India Narendra Modi na waziri mwenzake wa mambo ya nje Subrahmanyam Jaishankar.
 
Uhusiano wa Marekani na India kihistoria umekuwa wa misukosuko lakini suala la China kuzidi kujiingiza katika mgogoro na India kumeifanya Marekani na India kuwa karibu na hasa tangu mapigano makali yaliyosababisha umwagikaji damu mwaka jana katika mgogoro wa eneo la mpaka baina ya India na China la Himalaya. India ni sehemu ya ushirikiano na Marekani,Japan na Australia dhidi ya China.
 
Ingawa kuna hisia kwamba uungaji mkono wa Marekani kwa India chini ya utawala wa rais Joe Biden sio mkubwa kama ilivyokuwa chini ya Donald Trump ambaye maafisa wake waliikosoa waziwazi China na kuiunga mkono India katika mgogoro wake na China.

 

Chapisha Maoni

Mpya zaidi Nzee zaidi

Popular Items