Vyombo vya Habari nchini Haiti vimeripoti leo kuwa ofisi ya mwendesha mashtaka wa nchi hiyo imependekeza kushtakiwa kwa waziri mkuu wa mpito Ariel Henry kuhusiana na mauaji ya rais Jovenel Moise yaliyotokea mnamo mwezi Julai.
Taarifa hizo ni kulingana na barua iliyotumwa na ofisi ya
mwendesha mashtaka kwenda kwa jaji anayehusika na kesi ya mauaji ya rais
Moise ambayo imeorodhesha madai ya kuhusika kwa waziri mkuu Henry
kwenye mkasa huo.
Inaarifiwa kuwa serikali imetoa tangazo la kumfuta
kazi mwendesha mashtaka mkuu wa serikali baada ya ofisi yake kutuma pia
barua nyingine kwa mamlaka za uhamiaji ikimzuia waziri mkuu Henry
kuondoka nchini humo.
Hayo yanajiri baada ya vyombo vya habari kuripoti
kuwa hivi karibuni waziri mkuu Henry aliitwa mbele ya waendesha mashtaka
kutoa maelezo juu ya mawasiliano ya simu aliyoyafanya na moja ya
washukiwa wa mauaji ya rais Moise usiku wa siku ya shambulizi.
