Watu 50 waliokuwa wawazuia wahamiaji kuingia Ujerumani wakamatwa


 Polisi ya Ujerumani imewazuia zaidi ya watu 50 wanaounga mkono siasa kali za mrengo wa kulia waliojihami kwa pilipili ya kupuliza, bunduki, panga na rungu walipokuwa wakipiga doria mpaka wa Ujerumani na Poland ili kuwazuia wahamiaji wasiingie nchini humo. 


Watu hao walikuwa wanaitikia wito wa chama cha mrengo wa kulia Third Way kinachoshukiwa kuwa na mafungamano na makundi ya unazi mambo leo, ambalo liliwataka wanachama wake kusitisha uvukaji haramu wa wakimbizi karibu na mji wa Guben kwenye mpaka wa Ujerumani na Poland. 


Msemaji wa polisi amesema wamekamata silaha zilizokuwa zimebebwa na washukiwa hao na kuwaamuru waondoke katika eneo hilo huku baadhi ya watuhumiwa wakidaiwa kusafiri kutoka maeneo mengine ya Ujerumani kuja hadi kwenye mpaka wa Poland. 


Waziri wa mambo ya ndani wa Ujerumani Horst Seerhofer amesema tayari kulikuwa na kesi 6,162 za wahamiaji ambao hawajaidhinishwa kuingia Ujerumani kutoka Belarus na Poland mwaka huu.


Post a Comment

0 Comments