Watoto 400,000 kuwapa vyeti vya kuzaliwa Katavi, Rukwa

 


Zaidi ya watoto 400,000 walio na umri wa chini ya miaka mitano kutoka katika mikoa ya Katavi na Rukwa wanatarajiwa kusajiliwa na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa ndani ya mezi miwili ijayo.


Tofauti na awali wakati usajili na upatikanaji wa vyeti hivyo ulikuwa unafanyika kwenye ofisi za wakuu wa wilaya, kwa sasa uandikishaji na utoaji unafanyika bure kwenye ofisi za kata, zahanati na vituo vya afya mara mtoto anapozaliwa.


Uandikishaji huo unafanywa kwa ushirikiano ya Serikali ya Tanzania kupitia Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (Rita), Shirika la Kuhudumia Watoto Duniani (Unicef), Kampuni ya Simu za Mkononi ya Tigo na Serikali ya Canada.


Akizindua shughuli ya usajili na utoaji wav yeti hivyo, Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Paramagamba Kabudi amesema usajili kwa watoto umepanda kutoka asilimia 13 mwaka 2015 hadi kufika asilimia 65, mwaka huu.


Amesema mikoa ya Rukwa na Katavi, usajili umeanza kwa kuchelewa kwa sababu ya kiusalama kutokana na kuwepo kwake mipakani.


“Mikoa 20 imeshasajiliwa na hii ilinayopakana na nchi jirani ilikuwa lazima kusubiri utaratibu, usajili ni muhimu kwa sababu unaisaidia Serikali kufahamu idadi ya watu wake na kuweza kupanga shughuli zake za maendeleo ipasavyo,” amesema Profesa Kabudi.


Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Rita, Profesa Hamisi Dihenga amesema usajili na utoaji wa vyeti kwa watoto utazifanya mamlaka mbalimbali ikiwamo ya elimu, kuandaa mipango yake kwa miaka saba ijayo.


“Hata uandaaji wa madarasa hautakuwa wa kukurupuka, usajili huu unakufanya ujue miaka saba ijayo ni watoto wa ngapi wataanza darasa la kwanza hivyo hata madarasa yatakayo andaliwa kwa uhakika,” amesema Mrisho.


Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Ulinzi cha Mtoto kutoka Unicef, Maud Fortuyn amesema wanatamani kuona kila mtoto anayezaliwa Tanzania, anapata haki ya kusajiliwa na kupewa cheti.


“Kwa sababu usajili unafanyika kwa njia ya teknolojia, tunaamini utawafikia watoto wote, Unicef itaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania kuhakikisha kila mtoto anayezaliwa anasajiliwa,”amesema.


Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Joseph Mkirikiti amesema vyeti vya utambuzi kwa watoto wanaozaliwa kwenye mikoa hiyo ni muhimu kutokana na kuwepo kwake mipakani.

Post a Comment

0 Comments