Musoma kutumia Sh40 milioni kuanzisha kituo cha mitihani


 Manispaa ya Musoma mkoani Mara inatarajia kunzisha kutuo cha mitihani lengo likiwa ni kumaliza daraja sifuri kwa wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne katika manispaa hiyo.


Kituo hicho hadi kukamilika kinatarajiwa kugharimu zaidi ya Sh40 milioni ambapo fedha hizo zinatarajiwa kupatikana kutoka kwa wadau mbalimbali wa manispaa hiyo.


Akizingumza mjini hapa leo Januari 14, 2022 wakati wa makabidhiano ya madarasa yaliyojengwa na fedha za uviko 19, Meya wa Manispaa ya Musoma, William Gumbo amesema kuwa kituo hicho kinatarajiwa kuanza kufanya kazi mwezi Aprili mwaka huu.


Amesema kuwa uamuzi huo umetokana na ukweli kuwa wanafunzi wengi wamekuwa wakipata daraja sifuri na hivyo kusababisha kuendelea kuwepo kwa adui ujinga katika manispaa ya Musoma.


Amesema kuwa maandalizi ya kituo hicho tayari yameanza na kwamba ili kufaniksha jambo hilo mbunge wa jimbo la Musoma mjini, Vedastus Mathayo tayari amechangia kiasi cha Sh11.5 milioni kwaajili ya ununuzi wa mtambo mmoja wa kuchapisha mitihani.


"Tunatarajia kuwa na mitambo kama mitatu  hivi na kila mtambo utagharimu zaidi ya Sh11.5 milioni na fedha hizi tutazipata kutoka kwa wadau wetu na mbunge wetu tayari amefungua pazia kwa kutoa fedha kwaajili ya ununuzi wa mtambo mmoja" amesema Gumbo.


Ameongeza kuwa mbali na kituo hicho lakini pia wapo vijana sita ambao wamejitolea kwaajili ya kufundisha masomo ya sayansi katika shule za sekondari huduma ambayo itafanyika kwa mzunguko katika shule hizo.


Gumbo amefafanua kuwa ili vijana hao waweze kufanikisha lengo hilo mbunge huyo pia ametoa Sh6 milioni kwaajili ya kuwawezesha vijana hao kuweza kutoa huduma bila kikwazo.


Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Dk Halfan Haule amesema kuwa hali ya ufaulu kafika manispaa hiyo ni asilimia 86 huku wanafunzi zaidi ya 500 walipata daraja sifuri katika mtihani wa kidato cha nne mwaka jana.


Mbunge wa Musoma mjini, Vedastus Mathayo amesema kuwa kituo hicho cha mitihani kwa namna moja ama nyingine kinalenga kuunga mkono juhudi za serikali katika kuboresha elimu nchini.


"Kwakweli inasikitisha sana watoto takriban 1,000 kupata daraja sifuri hii inakatisha tamaa hata kwa wazazi kwani wamejitahidi kuwapeleka watoto shule kuanzia shule ya msingi lakini wanapofika kidato cha nne wanafeli hivyo inakuwa ni hasara kwa wazazi na jamii nzima," amesema

Post a Comment

0 Comments