Watano wahukumiwa Kifungo cha maisha jela kwa mauaji ya mtu mwenye ualbino Malawi

Watu watano akiwemo kasisi wa kanisa la katoliki wamehukumiwa kifungo cha maisha jela na kazi ngumu kwa kumuua mwanamume mwenye ualbino nchini Malawi miaka minne iliyopita.

Walipatikana na hatia ya kumuua MacDonald Masumbuka ambaye alitoweka Machi 2018 Kusini mwa Malawi.

Ni kesi iliyoshtua Malawi. Na sasa wauaji wa MacDonald Masumbuka watatumikia maisha yao yote gerezani kwa mauaji ya kijana huyo mwenye umri wa miaka 22 ambaye alikuwa na ualbino.

Watu wengine sita akiwemo polisi na ndugu wa mwathiriwa walihukumiwa kifungo cha kati ya miaka 30 na 60 jela kwa kosa la kufanya biashara haramu ya viungo vya binadamu.

Bw Masambuka alitoweka mapema Machi 2018, mwili wake ulipatikana wiki kadhaa baadaye ukizikwa kwenye kaburi lenye kina kifupi. Mauaji yake yalikuja wakati wa mashambulizi kadhaa dhidi ya zaidi ya watu arobaini wenye ualbino katika nchi hiyo ya Kusini mwa Afrika.

Zaidi ya kesi nyingine 20 za unyanyasaji dhidi ya watu wenye ualbino zinaendelea katika mahakama za Malawi. Mauaji hayo yanahusishwa na mila zinazohusishwa na uchawi, huku watendaji wakiamini kimakosa kuwa viungo vya waathiriwa vinaleta bahati nzuri.

 

Post a Comment

0 Comments