Mali yamfukuza mkuu wa kitengo cha haki za binadamu kwenye tume ya UN


Utawala wa kijeshi wa Mali Jumapili umesema kwamba umemfukuza mkuu wa kitengo cha haki za binadamu kwenye tume ya Umoja wa mataifa (MINUSMA), na kumpa saa 48 awe ameondoka nchini humo.


Uamuzi huo unajiri baada ya mwanaharakati wa haki za binadamu raia wa Mali kukosoa hali ya usalama nchini humo katika hotuba yake kwenye mkutano wa Umoja wa Mataifa na kuwashtumu washirika wapya wa kijeshi kutoka Russia kwa kuhusika na ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu.


Wizara ya mambo ya nje ya Mali imetangaza kuwa Guillaume Ngefa Atonodok Andali, mkuu wa kitengo cha haki za binadamu kwenye MINUSMA, anatakiwa kuondoka nchini humo, imesema taarifa iliyotolewa na msemaji wa serikali, Kanali Abdoulaye Maiga.


“Hatua hii inajiri baada ya vitendo vya kukera na visivyoridhisha vya bwana Andali, “ taarifa hiyo imeongeza, ambayo ilisomwa pia kwenye habari za televisheni ya taifa.


Andali alijipa jukumu la kuamua ni nani wawakilishi wa mashirika ya kiraia, akipuuza mamlaka na taasisi za taifa, taarifa ya serikali imeongeza.


“Kuegemea upande mmoja kwa Andali kulidhihirika zaidi wakati wa ukaguzi wa siku za nyuma wa Baraza la Usalama la Umoja wa mataifa kuhusu hali ya Mali,” taarifa hiyo imeongeza.

Post a Comment

0 Comments