Watumishi Ofisi ya Waziri Mkuu watakiwa kufanya kazi kwa ushirikiano



Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulika  masuala  ya  Sera Bunge na Uratibu Dkt. John Jingu, amewataka watumishi wa Ofisi hiyo kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuwa na utendaji wenye matokeo.

Dkt. Jingu  ameyasema hayo wakati wa mkutano wa watumishi wa ofisi yake uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi uliopo Njedengwa Jijini Dodoma  ambapo ulilenga  kuwajengea uelewa kuhusu mada masuala ya Afya ya akili, magonjwa sugu yasiyoambukizwa na ulaji usiofaa pamoja na maadili mahali pa kazi.

Katibu Mkuu  aliwasisitiza  watumishi kutekeleza majukumu yao kwa weledi na ufanisi kwa kushirikiana ili kuyafikia malengo ya serikali kwa ujumla na kujiletea maendeleo.

Alisema kuwa ipo haja ya kuwa na mafunzo kwa kila mtumishi kwa kada zote ili kuwajengea uwezo utakaoleta tija katika kutekeleza majukumu yao.

“Inatubidi tufanye mafunzo ya muda mfupi katika vitengo na idara ili watu wapate ujuzi na hili ni jambo la muhimu katika kutusaidia kuongeza ufanisi na tija katika kazi,” alisema Dkt. Jingu.

Alifafanua kuwa, vikao vya idara na vitengo kila wiki vitasaidia kuwa na uelewa wa pamoja juu ya majukumu tuliyonayo ambayo yatasaidia kuongeza ushirikiano na uwezo katika utendaji kazi wa kila siku.

 “Lazima twende pamoja ili tufanye kazi kama timu, ili kuweza kufikia malengo, ambapo kuna malengo ya mtu binafsi na kuna malengo ya kiofisi, ustawi wa mtu mmoja ni muhimu katika kufanikisha malengo ya Ofisi na Serikali kwa ujumla”. Alisisitiza.


Kwa upande wake Mwenyekiti wa TUGHE, Tawi la Ofisi ya Waziri Mkuu Bi, Numpe Mwambenja ameishukuru ofisi kwa kuandaa mkutano huu wenye tija huku akisisitiza watumishi kuendelea kutekeleza majukumu kwa ushirikiano ili kuweza kutimiza malengo.

“Muongozo wa ugawaji wa majukumu ya utendaji kazi utasaidia kuongeza bidiii zaidi katika utendaji wa kazi wa kila siku na kutusaidia kupima utendaji wetu,”alisema Numpe.

Post a Comment

0 Comments