Oryx Gas na Doris Mollel Foundation wakabidhi mitungi ya gesi ya kupikia kwa wauguzi


KAMPUNI ya Oryx Gas na Taasisi ya Doris Mollel Foundation wamekabidhi mitungi ya gesi ya kupikia ya Oryx 50 kwa wauguzi katika Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala jijini Dar es Salaam kati ya mitungi  1000  inayotarajiwa kukabidhiwa kwa wauguzi na madaktari katika mikoa 10  nchini .

Akizungumza wakati wakisaini makubaliano ya ushirikiano yaliyofanyika katika hospitali ya rufaa ya Mwananyama, Mkurugenzi wa Kampuni ya gesi ya Oryx Gas Araman Benoite amesema makubaliano walioingia baina ys kampuni hiyo na taasisi ya Doris Mollel ni kusaidia kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa watanzania.

Aidha amesema katika kampeni hiyo ya kuwezesha watanzania kuingia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia, mpaka sasa tayari wameshatoa mitungi kwa wananchi zaidi ya elfu 32 ili kusaidia lengo la kufikia asilimia 80 ya watumiaji wa nishati safi.

Amesema matumizi ya nishati safi ya kupikia inasaidia kuondoa hatari za kiafya kwa watumiaji wa kuni na mkaa kama nishati ya kupikia lakini pia hatari za kimazingira na ustawi wa jamii.

"Takribani watu 33,000 wanapoteza maisha nchini Tanzania kwa maradhi yanayotokana na kuvuta moshi unaotokana na mkaa au kuni hiyo ndio sababu ya Oryx gas kuja na suluhisho la kuwahamasisha wananchi kutumia gesi kwa matumizi ya kupikia", amesema Benoite


Ameeleza kuwa matumizi ya gesi yanaepusha wamama na watoto kuumika kubeba kuni hivyo kuepuka kujeuriwa na wanyama wakali wakiwa katika harakati za kutafuta kuni pia kuimarisha maisha ya wanawake na kuwalinda dhidi ya vitendo vya udhalilishaji.

“Kuanzia mwezi wa saba mwaka 2021 tumekuwa mstari wa mbele kuunga mkono utekelezaji wa mkakati wa serikali uliopewa nguvu na Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania , Dk. Samia Suluhu Hassan kwa lengo kwamba ifikapo mwaka 2033 asilimia 80 ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia”, ameeleza.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya Doris Mollel , Doris Mollel amesema katika makubaliano waliosaini na oryx watawafikia waguzi elfu moja ambapo watawapa mitungi na majiko ya gesi kama mabalozi kwa kina mama waweze kutumia nishati safi ya kupikia ikiwa ni programu ya miaka miwili.

Amesema mitungi hiyo itakwenda kwa wauguzi walioko maeneo magumu ambapo watakuwa wanawatembelea kwenye vituo vya afya na zahanati ili kuweza kuwafikia wafanyakazi ambao ni wauguzi wanaofanya kazi kubwa ya kuokoa maisha hususani ya mama na mtoto.

Wakati huo huo Mganga Mfawidhi Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala  Dk.Zavery Benela ameeleza kwamba hospitali hiyo  inakabiliwa na ongezeko la wagonjwa wa mifumo ya hewa.

Amefafanua kati ya wagonjwa wa nje 500 wanaofika kuonwa na madaktari bingwa asilimia 30 ya wagonjwa hao ni wa matatizo ya mfumo wa hali ya hewa unaosababishwa na hali ya hewa pamoja na mazingira ya kuandaa chakula kutokna na kuni na mkaa.

Aidha Dokta Benela amesema magonjwa ya mfumo wa hali wa hewa  yamekuwa changamoto hasa kwa watu wazima na watoto.


 

Post a Comment

0 Comments