Waziri Jafo: watu milioni nne barani Afrika wanapoteza maisha kwa kutumia nishati chafu

 

Na Mwandishi Wetu, Arusha

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais,Muungano na Mazingira Dk.Selemeni Jafo amesema takwimu zinaonesha watu milioni nne barani Afrika wanapoteza maisha kwasababu ya kutumia nishati chafu ikiwemo ya kuni na mkaa.

Hivyo amesema ajenda ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ya kuanzisha kampeni ya kuhamasisha nishati safi Afrika inapaswa kuungwa mkono na watu wote  huku akitumia nafasi hiyo kueleza matumizi ya kuni na mkaa nchini yanasababisha hekta 46242 kupotea kila mwaka kwasababu ya kuni na mkaa.

Akizungumza leo Aprili 27,2024 wakati wa hafla ya kukabidhi mitungi ya gesi 1500 yakiwa na majiko yake kwa wananchi wa Jiji la Arusha wakiwemo wajasiriamali Dk.Jafo amesema hatua hiyo inakwenda kuunga mkono juhudi za Rais Samia katika kampeni ya kuhamasisha nishati safi.

“Rais Dk.Samia Suluhu Hassan amekuwa na dhamira njema na ndio maana amekuja na kampeni ya nishati safi ya kupikia.Haya ni mapenzi yake na kwasababu tunafahamu nishati chafu inamadhara makubwa katika mazingira.

“Kwanza watu wanalazimika kutegemea kuni na mkaa kwa hiyo kuna uharibifu wa mazingira.Takwimu zinaonesha kila mwaka hekta 46242 zinapotea kwasababu ya kuni na mkaa,”amesema Dk.Jafo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya gesi ya Oryx Benoite Araman amesema madhara yanayotokana na kutumia kuni na mkaa yamekuwa yakisababisha  wananchi 33,000 nchini Tanzania kupoteza maisha kila mwaka kwa kuvuta moshi na chembe chembe zinazotokana na mkaa na kuni.


Hivyo amesema kupika na gesi ya Oryx linakwenda kuokoa maisha ya watu ambao wataachana na kutumia kuni na mkaa na hivyo kuwa salama kiafya huku akisisitiza kutumia nishati safi ya kupikia kunasaidia kuzuia ukataji miti na hivyo husaidia kulinda mazingira.

Wakati huo huo Mbunge wa Arusha Mjini Mrisho Gambo amesema katika kuunga mkono jitihada za Rais Dk.Samia kuhamasisha nishati safi ya kupikia wameona ni vema kuendelea kuyagusa makundi mbalimbali katika jimbo hilo kwa kugawa mitungi ya gesi.

Amesema kuwa kabla ya kugawa mitungi hiyo 1,500 ya Oryx kwa wana Arusha Mjini, tayari ameshagawa pia mitungi 1400 kwa wajasiriamali huku akisisitiza wataendelea na kuyafikia makundi yote yakiwemo ya watoto wanaolelewa vituo vya ya watoto yatima.

Post a Comment

0 Comments