Na John Walter-Manyara
Klabu ya Fountain Gate Football Club (FGFC) imetangaza rasmi
kuhamisha makao makuu na kituo chake cha uendeshaji wa shughuli za klabu kutoka
Mkoa wa Manyara kwenda Mkoa wa Arusha, hatua inayofungua ukurasa mpya katika
historia ya klabu hiyo inayoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara.
Kupitia taarifa yake rasmi, uongozi wa Fountain Gate FC
umetoa shukrani za dhati kwa wakazi wa Mkoa wa Manyara, hususan wananchi wa
mjini Babati, mashabiki waaminifu, wadau na viongozi wa serikali kwa
ushirikiano mkubwa na mchango mkubwa walioutoa tangu klabu hiyo ilipoanza
kutumia Uwanja wa Tanzanite Kwaraa kama uwanja wake wa nyumbani.
Uongozi wa klabu umeeleza kuwa kipindi chote walichokuwepo
Manyara kimekuwa cha mafanikio, yakichangiwa kwa kiasi kikubwa na sapoti ya
jamii ya Babati ambayo ilijitokeza kwa wingi, ikiwemo kusafiri na timu kwenda
mikoa mbalimbali ilipokuwa ikicheza mechi zake za Ligi Kuu.
Sababu za kuhamia Arusha zimeelezwa kuwa ni pamoja na
kufungua fursa zaidi za kibiashara na uwekezaji, pamoja na sababu za kiufundi,
hususan upatikanaji wa miundombinu bora kwa ajili ya maendeleo ya timu.
Hata hivyo, uongozi wa FGFC umefafanua kuwa Mkoa wa
Manyara utaendelea kuwa makao ya Taasisi ya Fountain Gate, ambapo timu za
vijana na timu ya wanawake zitaendelea kutumia miundombinu ya michezo ikiwemo
Uwanja wa Tanzanite Kwaraa kwa ajili ya mafunzo na mashindano yao.
Aidha, klabu imetangaza kuwa tarehe 06 Februari 2026,
Fountain Gate FC itapokelewa rasmi Mkoani Arusha katika hafla itakayofanyika
chini ya uongozi wa Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha kuanzia saa 5:00 asubuhi.
Hatima ya Uwanja wa Tanzanite Kwaraa Babati
Baada ya kuondoka kwa Fountain Gate FC, Uwanja wa
Tanzanite Kwaraa uliopo mjini Babati sasa unabaki bila timu ya Ligi Kuu
itakayoutumia kama uwanja wa nyumbani. Hali hiyo imeibua maswali mengi miongoni
mwa wadau wa michezo na mashabiki wa soka mkoani Manyara.
Maswali yanayoibuka ni pamoja na:
- Je,
uwanja huo utatumika kwa shughuli zipi sasa?
- Ni
timu zipi zitapewa nafasi ya kuutumia?
- Je,
kuna mpango wa kuhamishia timu nyingine ya ligi kubwa mjini Babati?
- Hatima
ya mashabiki waliokuwa wakijitokeza kwa wingi kuujaza uwanja huo
itakuwaje?
Kwa sasa, mamlaka za michezo mkoani Manyara bado hazijatoa
kauli rasmi kuhusu mustakabali wa Uwanja wa Tanzanite Kwaraa, lakini wachambuzi
wa soka wanaona kuwa hatua hiyo ni changamoto na pia fursa ya kuendeleza soka
la mkoa huo kupitia timu mpya au uwekezaji wa kimichezo.

0 Maoni